
Akizungumza na wanafunzi wa skuli zilizoshiriki mashindano ya masomo
ya Sayansi kwenye fainali iliyozikutanisha Skuli ya Mikindani na Fidel
Castro katika Ukumbi wa Kariakoo, Waziri Riziki alisema masomo ya
sayansi yana umuhimu mkubwa katika karne ya sasa ya Sayansi na
Teknolojia.
Amesema kutokana na umuhimu huo Jumuiya ya kuhamasisha watoto wa kike
kusoma masomo ya Sayansi (FAWE) inachukua juhudi ya kuwashajihisha
kuyapenda masomo hayo.
Alisema hivi sasa Tanzania inaelekea katika uchumi wa viwanda na
wataalamu wa sayansi katika fani mbali mbali watahitaji hivyo upo
umuhimu mkubwa kwa wanafunzi wa kike kujikita katika masomo ya Sayansi
na Teknolojia.
“Tunahitaji wataalamu wa kike kwenye uvumbuzi wa mafuta na gesi,
walimu wa kufundisha masomo ya Sayansi, mafundi mitambo wa viwandani,
lazima mufuzu katika masomo ya sayansi,”alisisitiza Waziri wa Elimu.
Allishukuru Jumuiya ya FAWE kwa jitihada wanazochukuwa kwa
kuwahamasisha watoto wa kike kusoma masomo haya wakielewa kwamba
unapomuelimisha mtoto wa kike ni sawa na kuielimisha jamii.
Waziri wa Elimu aliwapongeza wanafunzi wa skuli ya Fidel Cstro Pemba
na Mikindani ya Unguja kwa kuingia fainali katika mashindano hayo
yaliyoshirikisha skuli kumi za Unguja na Pemba.
Aliahidi Wizara yake itaongeza mashirikiano na FAWE ili iweze
kuleta mabadiliko makubwa zaidi kwa wanafunzi wa kike na wanawake
walioko katika mazingira magumu ambapo ndio lengo kuu la Jumuiya hiyo.
Waziri Riziki aliwashukuru Milele Foundation kwa kuzifadhili skuli
zote 10 zilizoshiriki mashindano hayo na kusaidia ujenzi wa madarasa
skuli mbali mbali.
Mratibu wa Jumuiya ya FAWE Hinda Abdullah Ajmy alisema wameweka
mikakati ya kuandaa mashindano ya aina hiyo kwa lengo la kuongeza
nguvu katika kuibua vipa kwenye masomo ya sayansi.
Afisa mipango wa mradi wa Mradi wa Masomo ya Sayansi, Teknolojia,
Ufundi na Hesabati (STEM) Warda Mustafa Hamid alisema lengo la mradi
huo ni kuhamasisha wanafunzi waweze kusoma sayansi na kuwajengea uwezo
kuhamasisha wenzao .
Katika fainali hiyo skuli ya Fidel Castro ya Pemba imeshika nafasi ya
kwanza kwa kupata alama 55 na Skuli ya Mikindani Unguja imepata alama
48.07 na kushika nafasi ya pili.
chanzo:Zanzibar24
Comments