
Uongozi huo ukasema umefanya utafiti mdogo na kubaini chanzo cha
kuibuka majaa hayo na kuzagaa ovyo kwa uchafu kila kona ya kijiji hicho
kilichoko kwenye ukanda wa utalii.
Rais alitoa agizo hilo katika hutuba yake ya majumuisho kufuatia
ziara ya kikazi aliyoifanya Mkoa wa Kaskazini Unguja, ikiwa miongoni mwa
ziara zake za mikoa yote ya Zanzibar.
Lakini licha ya agizo la kiongozi wa juu wa nchi, bado kijiji hicho
kinasikitisha kutokana na taka nyingi zinazochafua mandhari ya eneo
hilo ambalo sasa ni miongoni mwa vivutio vikubwa vya utalii nchini.
Uchunguzi umebaini kwamba kiwango kikubwa cha taka zinazozagaa kwenye
majaa na ufukwe wa Nungwi, ni mifuko meusi ya plastiki iliyopigwa
marufuku hapa Zanzibar.
Mifuko hiyo hupatikana katika maduka, ikitumika kutilia bidhaa
zinazonunuliwa na wateja mbalimbali ambao hatimaye huitupa popote bila
kujali kuwa kufanya hivyo kunachafua mazingira na kuitia nchi aibu
machoni mwa watalii wanaotembelea ukanda huo.
Kiona mbali kimefurahishwa na hatua zinazochukuliwa sasa na uongozi
wa Halmashauri ya Wilaya hiyo katika kuhakikisha mazingira na maeneo
yake yanakuwa safi.
Lakini haikufurahishwa na kitendo cha kutokuona wajibu huo mpaka pale
Mhe. Rais alipoiona hali hiyo na kuweka wazi namna alivyokerwa na hivyo
kuuagiza uongozi wa halmashauri kulishughulikia tatizo hilo.
Katika hali ya kawaida, na kwa viongozi wanaojali majukumu yao,
Nungwi haikupaswa kufikia kiwango hicho cha uchafu kwani mji huo sasa
umekua kiuchumi na kibiashara na una vyanzo vingi vya mapato.
Kwa hivyo, sidhani kuwa ukosefu wa fedha unaweza kutajwa kuwa ni
sababu ya kushindwa kusimamia suala la usafi kijijini hapo, kwani kama
ni vifaa vinaweza kupatikana kwa kiwango cha kutosha.
Katika dhana ya uwajibikaji uliotukuka, haiingii akilini kwamba
uchafu na majaa hayo yangesubiri ujio wa mkubwa wa nchi kuyatolea agizo
ili yasafishwe.
Je, ingekuwaje kama kiongozi huyo hakuwa na ratiba ya kuzunguka
mikoani kwa sasa na miezi kadhaa mbele? Ndio kusema viambo hivyo
vingeliendelea kunuka uvundo utokanao na taka majaani zikiwemo za
masalia ya samaki ikizingatiwa eneo hilo lipo karibu na soko?
Ikumbukwe kuwa hali hiyo si ya leo wala jana, bali ni ya siku nyingi,
hivyo inasikitisha kwamba pamoja na mamia ya macho yanayoona hakuna
hatua yoyote iliyochukuliwa hadi Mhe. Rais alipofanya ziara kijijini
hapo.
Ifahamike kuwa halmashauri zina viongozi na watendaji wengi zikiwemo
kamati za mazingira, na hizi ni miongoni mwa kazi zao ambazo hazihitaji
kusubiri kumurikwa na ‘Kiona mbali’ au agizo la mkubwa pale anapofanya ziara za kikazi.
Uwajibikaji (Accountability) bila kusukumwa kwa amri na maagizo ya
viongozi wa juu ndio unaoonesha taswira ya aina ya kiongozi aliyepewa
dhamana ya kusimamia mambo kwenye eneo fulani.
Kushindwa kusimamia majukumu ambayo kwayo mtu analipwa kwa ajili ya
kuyetekeleza, kunawapa mwanya watu wengine wanaozitamani nafasi hizo
kulalamika pembeni na kumteta vibaya.
Na katika hali kama hii, iwapo mtu ataondoshwa kwenye wadhifa alionao, wa kulaumiwa ni yeye mwenyewe na asije kutafuta mchawi.
Kazi ya ‘Kiona mbali’ ni kuonesha njia kwa
yeyote anayekengeuka ili ajirekebishe, atekeleze na kusimamia vyema
wajibu wake na kutambua kwamba cheo ni dhamana na sio njia ya kuvuta
hela bila kutoka jasho.
Chanzo: zanzibar24.
Comments