Mkurugenzi wa Kinga na Elimu ya Afya Dkt. Fadhil Mo’hd Abdalla amesema iko haja kurejea utaratibu wa kizamani , wataalamu wa afya ya kinywa na meno kutoa huduma za matibabu katika maeneo mbali mbali ikiwemo maeneo ya maskuli na vijijini .
Hayo aliyaeleza katika Kituo cha Afya Rahaleo, wakati akifungua zoezi la uchunguzi wa afya ya kinywa na meno linaloendeshwa na Chama cha Madaktari wa Kinywa na Meno kutoka Tanzania .
Alisema afya hiyo ni muhimu kufanyika awali kabla ya madhara, kwa kupatiwa ushauri wa mapema kabla ya athari kujitokeza na kusababishwa kupoteza meno .
Alifahamisha kuwa katika miaka ya nyuma elimu ya afya ya kinywa na meno zilikuwa zikitolewa katika maskuli ,wataalamu hutoa elimu kwa wanafunzi pamoja na kung’oa meno kwa wale ambao meno yao yameadhirika .
“Huu usiwe mwanzo wa kuonyesha njia kwa jamii na wala msisubiri kuumwa kila muda mujiwekee utaratibu wa kujichunguza afya zenu ikiwemo afya ya kinywa na meno pamoja na maradhi yasioambukiza ili muweze kupata ushauri mapema kwa Madaktari ,”alisema Mkurugenzi Kinga .
Alieleza kutoa elimu na uchunguzi wa afya kwa jamii itasaidia kupunguza gharama za matibabu na kuimarisha kinga ya awali na kujiepusha na matumizi ya vyakula ambavyo vinachangia kuleta madhara ikiwemo vyakula vya sukari kuchangia uozeshaji wa meno hasa kwa watoto .
Nae Mwenyekiti wa Chama cha Madaktari wa Afya ya Kinywa na Meno ( TBA) Dkt Lorna Carneiro alisema mara hii wamepata fursa ya kuja Zanzibar kwa kufanya uchunguzi wa afya ya kinywa na meno ili kujua wale wagonjwa ambao wanamatatizo na kuwapatia tiba pamoja na kuwapa elimu ya afya .
Alisema Chama hicho kinahimiza umuhimu wa afya bora kwa jamii na kutoa ushauri wa maradhi mbalimbali ikiwemo ukimwi ,saratani ,Kifua kikuu,afya ya kinywa na meno pamoja na maradhi yasioambukiza kwa kuifanya jamii ipate uelewa na kujikinga na maradhi ambayo yanauwezo wa kuepukika .
“Hali ya idadi ya Wagonjwa ni kubwa wakati ya kuwa magonjwa haya yanakingika kwa haraka na kupona lakini kikwazo ni kuwa na uchache wa madaktari ,“alisema Dr Lorna .
Alifahamisha kila ifikapo tarehe 20 machi ya kila mwaka huadhimisha siku ya afya ya kinywa na meno kwa mwaka ujao wanatarajia uzinduzi wa zoezi hilo litafanyika Zanzibar .
Nae Mgonjwa BI Nargisi Uzia ambae alifika kupatiwa huduma ya matibabu katika kituo hicho alisema anaishukuru Serikali kwa kuwaletea wataalamu wa kuchunguza afya zao lakini pia iko haja ya zoezi hilo liwe endelevu kwani matatizo yako mengi yanahitaji uchunguzi.





chanzo:Zanzibar24
Comments