Dk. Shein-Hatuna sababu ya kushindwa kutoa elimu bure.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ametangaza rasmi kuwa kuanzia tarehe 1 Julai mwaka 2018 Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itatekeleza elimu bure kwa skuli za Sekondari za Serikali ambapo michango yote iliyokuwa ikitozwa kwa wazazi na wazee haitokuwepo tena.

 Dk. Shein aliyasema hayo leo katika kilele cha Sherehe za Tamasha la Elimu Bila ya Malipo zilizofanyika katika uwanja wa Gombani, Wilaya ya Chake Mkoa wa Kusini Pemba na kuhudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid, Mawaziri na viongozi wengine wa Serikali pamoja na wananchi na wanafunzi kutoka Unguja na Pemba.


 Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa kuanzia Bajeti ya mwaka 2018/2019 Skuli zote za Serikali za Sekondari zitatoa elimu bila ya malipo ambapo kwa kufanya hivyo ile azma ya Marehemu Mzee Abeid Amani Karume ya elimu bure itakuwa imekamilishwa.

Aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inao uwezo huo na ndani ya Bajeti yake bila ya kumkopa ama kumuazima mtu na hiyo ndio ahadi yake na ataitangaza rasmi siku itakapoanza kutekelezwa rasmi.

“Hatuna sababu ya kushindwa kutoa elimu bure iwe ya Maandalizi, Msingi ama Sekondari na naiagiza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali pamoja na Wizara ya Fedha na Mipango wawe makini sana katika kuipanga Bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali ya mwaka 2018/2019”,alisema Dk. Shein.

 Aidha, Dk. Shein alisema kuwa kwa upande wa elimu ya Juu utaratibu wa kutoa mikopo utaendelea kama ilivyo hadi pale zitakapofanywa taratibu nyengine.

Alieleza kuwa ni dhahiri kwamba katika kipindi cha miaka 53 ya Mapinduzi mafanikio makubwa yamepatikana katika kuyatekeleza malengo ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 ambapo katika kipindi chote hicho Serikali imeendelea kutoa elimu bila ya malipo ingawa si kwa kile kiwango cha miaka 15 ya mwanzo baada ya Mapinduzi.

Alisema kuwa hatua hiyo inatokana na sababu za matatizo ya uchumi na ongezeko la idadi ya watu yaliokumba nchi ambapo Serikali ililazimika kuwaomba wananchi wachangie elimu kwa utaratibu maalum ulioandaliwa kuanzia skuli za Msingi hadi Sekindari.

Hata hivyo alieleza kuwa kuanzia Julai, 2015 suala la uchangiaji wa elimu katika skuli za Maandalizi na Msingi kwa Unguja na Pemba limeondoshwa na Serikali inatoa elimu ya Msingi bila ya Malipo kama ilivyoamuliwa baada ya Mapinduzi.

Dk. Shein alieleza mafanikio yaliopatikana ndani ya miaka 53 katika sekta ya elimu ikiwa ni pamoja na kujenga taasisi kadhaa, vyuo vya ufundi, vyuo vya amali na chuo cha elimu mbadala kwa Unguja na Pemba ambavyo ni vingi kuliko wakati wa ukoloni pamoja na kuwa na vyuo vikuu vitatu vinavyoendeshwa na Wazanzibari wenyewe pamoja na kuwagharamia wanafunzi wote kwa kuwapa mikopo nafuu.

Alieleza kuwa fursa za elimu kwa fani mbali mbali zimeongezeka ambazo hivi sasa zinafundishwa hapa hapa Zanzibar ambapo takriban wataalamu 1800 wa fani mbali mbali wanahitimu kwenye Vyuo Vikuu vya Zanzibar, mbali na Taasisi nyengine za elimu ya juu.

Aliongeza kuwa Serikali inazitambua changamoto za walimu na itaendelea kuchukua hatua katika kukabiliana nazo hatua kwa hatua ambapo vipaumbele vya Serikali kwa hivi sasa ni kuimarisha ubora wa elimu, miundombinu ya elimu kwa kujenga skuli mpya, kuyakamilisha majengo yaliojengwa na wananchi, kuzitengeneza skuli za zamani, kuzipatia skuli vifaa vya maabara, samani na vitabu.

Dk. Shein aliongeza kuwa Serikali inatambua mchango muhimu wa walimu katika kuimarisha maendeleo ya sekta ya elimu “ nakiri Walimu mnafanya kazi kubwa nzuri, jitihada zinachukuliwa na Serikali katika kuyaimarisha maslahi ya walimu ili kuwapa ari ya kutekeleza wajibu wenu wa kuwalea na kuwapa elimu watotio wetu ili wawe rasilimali bora zaidi ya kuchangia maendeleo ya nchi yetu na kuwa raia wema na wazalendo”,aliongeza Dk. Shein.

Dk. Shein alitoa pongezi kwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali pamoja na Waziri wa Habari,Utalii, Utamaduni na Michezo pamoja na watendaji wao wote  kwa kufanikisha Sherehe hizo.
Pia, Dk. Shein aliuhimiza uongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kuongeza jitihada na nguvu maalum katika kufanikisha michezo kwa kushirikiana na Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo.

Mapema Dk. Shein alipokea maandamano ya wanafunzi walioshiriki michezo ya elimu bila ya malipo mwaka huu wa Unguja na Pemba.

Nae Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma alieleza kuwa uongozi wa Wizarav yake taendelea kuimarisha sekta ya elimu na kuhakikisha kuwa juhudi zitaendelea kuchukuliwa katika kuhakisha walimu wanataoa elimu bora.

Pia, Dk. Shein aliwapongeza washindi na walioshindwa katika michezo mbali mbali na shughuli za sanaa za mwaka huu na kutoa zawadi kwa washindi mbali mbali wa michezo pamoja na kushuhudia mashindano ya michezo yakiwemo mbio za vijiti, mashindano ya watoto wa maandilizi walioonesha umahiri wao katika mbio za magunia na mbio za miguu mitatu. Sherehe hizo zilipambwa kwa nyimbo mbali mbali zilizoimbwa na wanafunzi.
chanzo: zanzibar24.

Comments