Waziri wa Kazi,Uwezeshaji,Wazee,Vijana,Wanawake na Watoto Maudline Cyrus Castico amewataka vijana nchini kusoma kwa bidii ili kwenda sambamba na soko la ajira lenye kutaka vijana wenye elimu, ujuzi na uzoefu.
Akizungumza katika halfa ya uzinduzi wa mafunzo ya uwanajenzi kwa vijana wa chuo cha utalii amesema kutokana na hali ngumu katika soko la ajira lazima kuwepo kwa watendaji wenye nguvu kazi kielimu na sifa zenye kukubalika katika soko la ajira.
Amesema katika soko la ajira wafanyakazi ni wajibu wao kutoa huduma bora kulingana na elimu pamoja na ujuzi walio nao na waajiri kutoa ajira ambapo amesema kiwango cha kazi hupimwa kutokana na elimu, ujuzi na uzoefu walionao vijana.
Hata hivyo amesema endepo vijana watakuwa na mazingira bora katika soko la ajira wataweza kutengeneza uchumi wa taasisi na taifa kwa maendeleo endelevu.
Aidha castico amesema licha ya hatua mbalimbali zinazochukuliwa na serikali kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali duniani kuhakikisha vijana wanakwamuka na tatizo la ajira bado kuna changamoto za muda mrefu kwa waajiri Zanzibar wamekuwa na kilio kwamba vijana wengi waliopo katika soko la ajira hawana sifa stahiki zinazohitajika katika soko na kuwa na wasiwasi na uimara katika taasisi zao.
Amefafanua miongoni mwa mapungufu hayo ni pamoja na elimu duni kwa vijana,kiwango kidogo cha ujuzi na uzoefu katika fani mbalimbali ambapo matokeo yake waajiri hutafuta wafanyakazi wa kigeni ili kuziba upungufu katika taasisi zao.
“kutokana na kasoro mbalimbali zinazotajwa na waajiri lazima nitapambana kuhakikisha vijana wa Zanzibar wanasoma na kupata ujuzi wa fani mbalimbali ili kuuzika katika soko la ajira na kwa hawa vijana walioingia katika mafunzo haya ya uwanajenzi wataandaliwa vyema ili kuondoa kasoro zilizopo”amesema Castico.
Kwaupande wake Mwakilishi kutoka shirika la kazi duniani ILO Ashwani Aggrwal amesema kutokana na umuhimu wa ajira nchini shirika la kazi limekuwa likiweka mikakati na misaada ya kitaalamu na fedha kuzisaidia nchi mbalimbali duniani ili kukuza ujuzi kwa vijana ikiwa lengo ni kuwepo kwa sifa stahiki katika soko la ajira ili vijana kuweza kujiajiri wenyewe na hata kuajiriwa.
Hata hivyo ameeleza kuwa Programu hiyo ya mafunzo kwa vijana ni miongoni mwa hatua za kuwajengea mazingira bora vijana na kuwajengea daraja madhubuti katika ulimwengu wa kazi na mafunzo ili kuwepo kwa uwiyano mzuri baina ya ujizi na mahitaji ya soko au taasisi nchini.
“Tutadumisha ushirikiano wetu na serikali ya mapinduzi ya Zanzibar katika kuwajenga vijana mbalimbali duniani ili wende sambamba na soko na lengo letu hasa ni kupunguza wimbi la vijana walio mitaani kuweza kujiajira kwa fani mbalimbali hata za ujasiriamali”
Nae Mkurugenzi kutoka chuo cha utalii Zanzibar SUZA Aley Soud Nassor ametoa wito kwa serikali pamoja na shirika la kazi duniani kuwa bega kwa bega na walengwa wa mafunzo hayo ili fursa hiyo iweze kudumu na kuweza kuwafikia walengwa waliokusudiwa ili kuweza kunufaika na program hiyo.
Wakati huo huo Mwanafunzi kutoka chuo cha utalii aliyekuwepo katika program ya mafunzo hayo ya uwanajenzi Asia Salum Omar akisoma risala ya wanafunzi amesema wamefarajika na ujio wa mafunzo ambayo yatawajenga ili kuingia katika soko la ushindani ili kupata ajira lakini amesema tatizo kubwa linalowakabili wanapokwenda kufanyakazi kwa vitendo katika mahoteli kutoruhusiwa kuvaa mitandio kwa wanawake jambo waliloomba kutafutiwa ufumbuzi na serikali kuliingilia kati ili kuweze kudumishwa kwa mavazi ya kizanzibar katika sehemu za kitalii.
Aidha ameitaka serikali kwa kushirikiana na wadhamini kuwaendeleza vijana kielimu zaidi kutoka ngazi ya cheti hadi kufikia Digrii.
“Tunaamini utalii wetu wa Zanzibar utaendana na historia yetu kwani tusidumishe mavazi yetu ili twende sambamba na mila na desturi zetu kama wanavyofanya mataifa mengine duniani kudumisha mazehebu yao kwa mavazi”
chanzo:Zanzibar24
Comments