Serikali imezifungia shule 18.

Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni imezifungia shule za msingi na awali 18 kati ya 58 zilizobainishwa kutokuwa na usajili katika manispaa hiyo.

Zoezi hilo limesimamiwa na Kaimu Afisa Elimu wa Manispaa ya Kigamboni, Mwalimu Mathew Komba pamoja na Wakaguzi wa Elimu katika manispaa hiyo ambapo mapungufu mbalimbali waliyabaini kama shule kutokuwa na usajili, madarasa machache, kutokuwa na vyoo kwa ajili ya wanafunzi na walimu n.k.


Katika siku ya kwanza ya ukaguzi huo, timu hiyo imezifunga shule 18 kati ya 58 zilizobainishwa kutokuwa na usajili katika kata za Kigamboni, Vijibweni na Tungu.

Miongoni mwa shule zilizofungwa ni Malaika Nursery School, Kigamboni English Medium School, Patmos, Montecarlos, Riziki, Taqwa, Firdaus na Meck.

Hata hivyo, uongozi wa Manispaa ya Kigamboni imewataka wazazi kutowapeleka watoto wao kwenye shule hizo mpaka hapo watakapokamilisha taratibu walizowekewa ikiwemo kupata usajili.
chanzo: zanzibar24.

Comments