Dkt. Shein aahidi kuondoa kilio cha Wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, amewahakikishia wananachi wa kijiji cha Mbuyumaji na Mlilile Mkoa wa Kaskazini Unguja kuwa Serikali anayoiongoza itahakikisha inawapelekea huduma za afya, umeme, maji safi na salama, elimu na barabara ndani ya miezi sita ijayo.


Dk. Shein aliyasema hayo leo kwa nyakati tofauti mara baada ya kuvitembelea vijiji hivyo vilivyopo Wilaya ya Kaskazini A, ambapo aliwataka Mawaziri husika wa sekta hizo kuhakikisha huduma hizo muhimu zinawafikia wananchi hao katika kipindi hicho.

Dk. Shein alieleza kuwa kilio cha wananchi wa vijiji hivyo amekisikia na kuwaahidi juhudi za makusudi zitachukuliwa katika kuhakikisha huduma hizo muhimu zinapatikana.

Alieleza kuwa si jambo sahihi kuwepo kwa baadhi ya wananchi hapa Zanzibar kuendelea kukosa huduma hizo muhimu hivyo, alisisitiza kuwa juhudi zitachukuliwa katika kuhakikisha hilo linafanikiwa.

Nao Mawaziri wa sekta hizo pamoja na Mawaziri wengine aliofuatana nao Dk. Shein, waliahidi kutekeleza agizo hilo kwa wakati na kutumia fursa hiyo kumpongeza Dk. Shein kwa juhudi zake anazozichukua katika kuwaletea maendeleo wananchi wote wa Zanzibar bila ya ubaguzi.

Walieleza kuwa maendeleo hayana chama kwani yanamgusa kila mtu na kusisitiza kuwa wao wakiwa viongozi licha ya kuwa baadhi yao si viongozi kutoka CCM lakini watahakikisha wanamuunga mkono Dk. Shein na Serikali yake katika kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar.

Wananchi wa maeneo hayo walielezea kufurahishwa kwao na ziara ya Rais wa Zanzibar na kueleza matumaini yao makubwa kutokana na ziara hiyo ya Dk. Shein katika vijiji vyao na kufarajika na ahadi zake anazozitoa kwa lengo la kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020.

Mapema Dk. Shein alianza ziara yake katika Wilaya hiyo ya Kaskazini A, kwa kuweka jiwe la msingi katika Mradi wa Soko la Kinyasini na kuwaeleza wananchi kuwa Serikali inayoongozwa na CCM kwa mashirikiano ya washirika wa maendeleo ndio wanaojenga soko hilo na sio mwengine.

Dk. Shein alieleza kuwa wananchi walio wengi watafaidika na ujenzi wa soko hilo kwa kupata ajira sambamba na kuwa na sehemu nzuri ya kufanyia biashara ambapo maisha yataimarika kwa familia nyingi zitakazotumia soko hilo.

Aidha, Dk. Shein alieleza kutoridhika kwake na hali ya baadhi ya wafanyabiashara hivi sasa kuuza mazao yao pembezoni mwa barabara katika eneo hilo la soko na kueleza kuwa jambo hilo sio muwafaka.

Pamoja na hayo, Dk. Shein aliwahakikishia wananchi wa kijiji hicho cha Kinyasini kuwa Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya Bububu Mkokotoni ambayo itaanzia Chuini na kuwa si muda mrefu ujenzi wake utaanza na kuweza kuwasaidia sana wananchi wakiwemo wa kijiji hicho na  maeneo mengine ya Mkoa huo.

Uongozi wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi na kupitia Programu ya Miundombinu ya Masoko, Uongezaji Thamani na Huduma za Kifedha Vijijini (MIVARP) inayogharamiwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) ulieleza kuwa mradi wa ujenzi wa soko hilo utagharimu TZS Bilioni 2.5.

Uongozi huo ulieleza kuwa soko la Kinyasini ndio soko kubwa  kati ya masoko yote yanayojengwa kupitia mradi wa MIVARF na kueleza kuwa kazi inayoendelea hivi sasa ni ujenzi wa masoko ya Kinyasini Unguja, Tibirinzi Chake Chake Pemba na soko la Konde na ukarabati wa soko la mbogamboga Mombasa na ujenzi wa kituo cha mafunzo ya uhifadhi na kupunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno huko Pujini Pemba.

Mara baada ya kuweka jiwe la Msingi na kupata maelezo katika kituo cha uokozi na uzamiaji kiliopo Nungwi Dk. Shein alitoa pongezi kwa kuanza vyema mradi huu wa ujenzi wa vituo vya uokozi na uzamiaji.

Aidha, Dk. Shein alitoa pongezi zake kwa Mkuu wa Kikosi hicho cha KMKM kwa kukiendeleza vyema kikosi hicho huku akisisitiza kuwa nia ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni ya kukifanya kikosi hicho kuwa cha kisasa zaidi.

Mapema Katibu Mkuu Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Radhia Rashid Haroub alieleza kuwa Mradi huo umeanza rasmi mwaka 2014/2015 na unatarajiwa kukamilika mwaka 2018/2019.

Alieleza kuwa kukamilika kwa mradi huo utajumuisha ujenzi wa vituo sita ambapo hadi sasa kituo kimoja cha KMKM Kibweni kimekamilika na KMKM Nungwi kimo katika hatua za mwisho.

Pia, umo ununuzi wa vifaa vya mawasiliano kwa vituo vyote tayari umekamilika, utoaji wa mafunzo kwa wazamiaji 48 kati ya 62 yamekamilika na mafunzo kwa wadau watumiaji bahari.

Pamoja na hayo, Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa katika kutekeleza ununuzi wa Boti katika mradi huo Serikali imetenga TZS 2.1 Bilioni kwa ununuzi wa boti mbili mpya za kisasa zenye uwezo wa kuokoa na kutoa visaidizi 600 kwa wakati mmoja kwa chombo kimoja.

Katika ziara yake hiyo pia, Dk. Shein aliweka jiwe la msingi katika Maskani ya CCM Tushikamane na kusalimiana na wanachama na wananchi katika eneo hilo na kuahidi kutoa mchango wake kwa kuliezeka pamoja na kuliweka madirisha na milango.

Akiwa katika eneo la Mkokotoni ambapo Serikali ina ampango wa kujenga bandari kwa ajili ya vyombo vya usafiri wa watu pamoja na bidhaa, Dk. Shein alipongeza hatua nzuri za matayarisho, bandari ambayo itakuwa na urefu wa mika 170 na urefu wa mita 6.

Kabla ya kuangalia eneo hilo la Bandari, Dk. Shein alikagua na kupata maelezo juu ya jengo la Ofisi ya Bandari hapo hapo Mkokotoni ambalo tayari ujenzi wake umekamilika.

Kwa mujibu wa maelezo ya uongozi wa Shirika la Bandari, ujenzi wa Bandari hiyo ya Mkokotoni hadi kumalizika kwake utakharimu jumla ya TZS Bilioni 1.8 ambapo ujenzi wa nyumba hiyo ya Shairika hilo umegharimu jumla ya TZS milioni 378.7.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
chanzo: zanzibar24.

Comments