Bodi ya udhamini ya jumuiya matumizi bora ya Maliasili kwa tarafa za Idodi na Pawaga (MBOMIPA) mkoani Iringa imevunjwa kwa kutosaidia wananchi na kufanya kazi kifisadi pamoja na kuvunja mikataba.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe ameivunja bodi hiyo alipokuwa kwenye ziara yake katika jumuiya hiyo ya MBOMIPA na kufanya mkutano na wajumbe wa Bodi hiyo kabla ya kuvunjwa.
Prof. Maghembe alisema anashangazwa kuona MBOMIPA inajiendesha kwa hasara na kuomba omba kwa wahisani fedha za kujiendesha wakati kimsingi asasi hiyo ilipaswa kuwa msaada mkubwa kwa wanachama wao ambao ni vijiji vinavyozunguka hifadhi hiyo.
“Hii ni aibu kubwa kwa chombo hiki ambacho kinapaswa kuwa msaada kwa jamii chenyewe kimegeuka kuwa ombaomba, hivi inawezekana vipi MBOMIPA kuomba hadi msaada wa sare na mataili mawili kwa wahisani. Hili ni jambo la aibu kiufupi halikubaliki hakuna cha mwekezaji hapa wala cha bodi tunaanza upya vitu vyote tunaanza sifuri,” alisema Prof. Maghembe.
“Tutajidanganya kabisa kusema kwamba tuendelee na bodi ya Mbomipa kama ilivyo tutajidanganya kabisa, kwahiyo kuanzia leo nimeivunja bodi ya MBONIPA rasmi leo hapa.”
Aidha Waziri Maghembe ameagiza taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU) kufanya uchunguzi na kuwachukulia hatua wote waliohusika na ufisadi katika bodi hiyo ya MBOMIPA.
chanzo:zanzibar24.
Comments