
Akizungumza katika Mkutano wa Uzinduzi wa Wasaidizi wa Kisheria
katika Wilaya ya Magharibi B, Mkuu huyo alisema iwapo kutakuwa na
mashirikiano ya pamoja kukabiliana na vitendo vya udhalilishaji bila
shaka vitendo hivyo vitakwisha.
Alisema ni vyema Shehia zinazopatikana katika Wilaya hiyo
anayoiongoza kuyaripoti matukio ya udhalilishaji kwa Wasaidizi wa
kisheria ili watekeleze majukumu yao ikiwa ni pamoja na kushirkiana na
Wanasheria katika kuzipekeka kesi mahakamani na kupatiwa ufumbuzi.
Alisema tatizo lililozoeleka ni jamii kuoneana muhali na kushindwa
kuzipeleka kesi hizo katika vyombo vya sheria jambo ambalo linapunguza
kasi ya mapambano ya udhalilishaji.
Mkuu huyo wa Wilaya alisema uzinduzi huo umefanyika wakati muafaka
ikiwa jamii bado inakabiliwa na tatizo la udhalilishaji na kwamba
Wasaidizi wa Kisheria wataweza kulipunguza tatizo pale watakapopewa
mashirikiano ya kutosha.
“Tukitumia sheria iliyopo tutafanikiwa kwani sheria ndio msingi wa
utatuzi wa suala hili tujitahidi kushirikiana katika kutoa ushahidi”
alisema Silima.
Alisema tabia iliyozoeleka kwa Jamii kuyamaliza nyumbani matatizo
ya udhalilishaji ni jambo linalochochea kwa kiasi kikubwa Wanafamilia
kuendelea kujihusisha na matukio ya udhalilishaji kwa kuamini kuwa
hawatachukuliwa hatua za kisheria.
Alifahamisha kuwa ili kushinda mapambano dhidi ya udhalilishaji
ambayo yamekithiri ni vyema kuondoa huruma na muhali kwa watu ambao
wanahatarisha maisha ya watoto kwa kuwafanyia matendo hayo.
“Ukweli ni kwamba udhalilishaji umekithiri hasa kwa watoto wa
jinsia zote tuwe na huruma kwa watoto wetu kuwafanyia vitendo hivi
kwani mtoto ukimfanyia kitendo hicho unamvunjia maisha yake kwa
kumuathiri kimwili na kisaikoloji hivyo tushikamane ili kuwashinda wale
wasiowatakia mema watoto wetu”Alisema Silima.
Nae Katibu wa Umoja wa wanasheria Wilaya ya Magharibi B Bimkubwa
Haji Kheir alisema uzinduzi wa Wasaidizi wa Sheria juu ya vitendo vya
udhalilishaji katika Wilaya hiyo utawajengea uwezo mkubwa Wanawake na
watoto kujua haki zao.
Akizungumzia kuhusu malengo ya uzinduzi wa mradi huo alisema ni
pamoja na kuwashajihisha wanajamii kuweza kufahamu uwepo wasaidizi wa
sheria katika wilaya na pindipo ikitokea kesi ya udhalilishaji
kukimbiliana kuwapatia msaada wa kisheria.
Hata hivyo ameyazungumzia malengo waliyojiwekea ni kuwawezesha
wanajamii kuifahamu na kuitambua sheria ya mtoto no 6 ya mwaka 2011 ili
kuweza kusimamia na kuitekeleza kwa maslahi ya mtoto.
Pia kuimarisha mawasiliano kati ya serikali za mitaa na mitandao ya
kijamii katika kukuza uelewa kwa jamii juu ya masuala ya maendeleo,
matunzo na afya bora kwa mtoto.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa chama cha wanasheria wanawake
Zanzibar ZAFELA Safia Hija Abras alisema, wanasheria wa zafela
wamefarijika sana kuwepo kwa wasaidizi wa kisheria ndani ya wilaya hiyo
kwani kutapelekea kuwasaidia akinamama wanaofanyiwa vitendo vya
udhalilishaji kupata urahisi wa kupeleka kesi zao kwa wasaidizi hao na
kushughulikiwa kiharaka.
Uzinduzi huo wa Wasaidizi wa Kisheria katika Wilaya ya Magharibi B
umefadhiliwa na LSF Ligo Service facilities kutoka Tanzania kwa msaada
wa Shirika la Danida, Ukaid kwa lengo la kutatua matatizo
yanayowakabili kinamama na watoto pamoja na walemavu.
chanzo: zanzibar24.
Comments