
Akizungumza katika kikao cha pamoja kilichowajumuisha watendaji wa tume
hizo, Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya kudhibiti Ukimwi Tanzania Dk.
Leonard Maboko amesema utafiti unaoendelea umeonesha kuwa vijana wenye
umri wa miaka 15-19 ndio wanaoathirika zaidi na maambukizi mapya,
hususani wanawake .
Akizungumzia hali ya maambukizi hapa Zanzibar Mkurugenzi mtendaji wa
Tume ya ukimwi Zanzibar Ahmed Muhammed Khatib amesema maambukizi hayo
kwa asilimia kubwa yanatoka katika makundi maalumu ikiwemo Wanawake
wanaouza miili yao , wanaume wanaojamiana bila ya kutumia
kinga na vijana waaotumia madawa ya kulevya hali inayochangia kuenea
kwa ugonjwa huo.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tume hiyo Dk. Hedwiga Swai amesema
kikao hicho kitakuwa chachu ya maendeleo juu ya kuhamasisha wananchi
kuitumia elimu wanayopewa na kutumia kinga wakati wa tendo la ndoa
hususani vijana ili kupunguza viashiria vya ugonjwa wa ukimwi katika
jamii.
Hata hivyo amesema utafiti unaoendelea inaonesha idadi ya maambukizi
imepungua ambapo kwa mwaka 2013 maambukizi hayo yalikua 72,000 na mwaka
2014 69,603 ,Mwaka 2015 48,000 na wito kwa jamii kuendelea kufuata
taratibu za kiafya zinazotowa na wataalamu wa afya ili kujikinga na
ugonjwa huo.
Naye Mwenyekiti Kamati ya Ushauri ya masuala ya UKIMWI, Afya ya kina
mama na Watoto ya Taasisi ya Mabunge Duniani (IPU) Dk. Faustine
Ndugulile amesema watahakikisha makubaliano hayo yanatekelezwa kwa
mahitaji yaliyokusudiwa pamoja na kuwa na mpango endelevu ya kuwa na
rasilimali fedha utakaowezesha kuondoa unyanyapaa kwa wagonjwa pamoja na
vifo vinavyosababishwa na Ugonjwa wa ukimwi.
Dk. Ndugulile amesema wataendelea kuishauri serikali kuelekeza nguvu
katika kuzisaidia taasisi na jumuiya zinazosimamia masuala ya ugonjwa wa
ukimwi ili jumuiya hizo ziweze kufikia malengo waliyoyakusudia na
kuwaokoa vijana ambao ni nguvu kazi ya taifa.
Mkutano huo wa siku mbili uliofanyika Maisara mjini Zanzibar
ulihudhuriwa na wajumbe wa kamati ya Bunge ya Masuala ya Ukimwi,
watendaji wa Tume za Ukimwi kutoka Tanzania Bara na Visiwani ukiwa na
lengo la kutafuta njia bora ya kuweza kupunguza kasi ya maambukizi ya
ugonjwa wa ukimwi.
chanzo: zanzibar24.
Comments