WAKULIMA
wa kilimo cha Shadidi katika bonde la Weni, Wilaya ya Wete, wanaendelea kupata
matumaini ya kujikimu kwa chakula baada ya kulima na kupata mavuno zaidi ya
mpunga wa umwagiliji maji msimu huu.
Wakulima hao walitoa maelezo kwa
nyakati tofauti, wakati walipokuwa katika ziara ya uvunaji wa pamoja katika
bonde hilo, huko Weni, Mkoa wa Kaskazini Pemba.
Waliendelea kueleza kuwa, kilimo cha
shadidi kwa sasa ndio mkombozi mkubwa kwa wanajamii kujitosheleza kwa chakula
na kuondokana na hali ngumu ya maisha, jambo ambalo linawekana kufuatia uwepo
wa wataalamu.
Mmoja kati ya wakulima wa kilimo cha
Shadidi, Bonde la Weni, Maryam Rashid Issa, alisema kuwa, jitihada inahitajika
katika kuendeleza kilimo cha mpunga, ili kupata tija kubwa kupitia mbegu kidogo
zenye kutoa mavuno mengi.
‘’Tujitahidini wakulima wenzangu
tusivunjike moyo, mavuno ni mazuri, mbegu kidogo lakini ndo kama mnavyoona,
tunawashukuru wataalamu wetu wakati wowote tunaowahitaji wanaitika’’, Mkulima
huyo alieleza.
Hata hivyo, mkulima kutoka bonde la
Dobi, Haji Mohammed Rubea ,alieleza kuwa uhalisia unaonesha wakati wa mavuno,
hivyo aliwataka wakulima wenzake kufanya ushindani wa mafanikio kwa kupeana
taaluma waliopatiwa kuendeleza mafanikio kwa faida yao na vizazi vijavyo.
‘’Mimi sijui siku niliokwenda dukani
tokea kuanza kilimo cha shadidi, mavuno ni mazuri na mengi pembe nalisikia
tu’’, alisema mkulima huyo.
Akisisitiza uendelezaji wa kilimo
hicho Afisa kilimo, Wilaya ya Wete, Makame Hamad Said, alisema kuwa, tofauti
kubwa ya mapato inaonekana wazi kwa wakulima kutokana na mavuno wanayoyapata
kulinganisha na kilimo cha kutegemea mvua.
‘’Mvuno ni mazuri sana, ni hatua
nzuri kufikia tani saba kwa hekta, ambapo kilimo cha kutegemea mvua huwezi
kufika hata tani moja pamoja na mvua nyingi zilizonyesha kwa msimu huu’’,
Makame alieleza.
Sambamba na hayo, Afisa huyo alisema
kuwa, hatua ya wakulima wa umwagiliaji maji imefikia pazuri kiasi cha kupewa
kipao mbele kwa kupatiwa pembejeo za kutosha, ili kutoa motisha kwa wakulima
hao.
‘’Mpunga kama mpunga ndio chakula
chetu, kiasi kwamba nyumbani kama hakuja pikwa wali huona hakuja pikwa,
tuendelee kuhamasishana kuhakikisha kilimo hichi kinaendelea hata kama hakuna
wahisani tuendeleleze taaluma tulionayo tuone vipi inazalisha kwa faida yetu’’,
afisa huyo alieleza.
Kwa upande wake, Afisa utafiti wa
Kilimo Pemba, Khatibu Bakar Haji, alisema kuwa, kupitia mbegu bora
zilizofanyiwa utafiti wa kina kupitia kilimo shadidi kuna uwezekano wa
kujitosheleza kwa chakula.
Sambamba na hayo, Afisa Mkuu Idara
ya umwagiliaji maji, Mbarouk Ali Mgau, alisema imani yake ni kuwa, wakulima
wengi wamepata mabadiliko baada ya kufuata maelekezo ya wataalamu, pamoja na
kuwataka waliopata hasara katika mavuno kuendeleza jitihada zao, ili waweze
kufikia malengo katika msimu ujao.
Mradi wa kuongeza zao la Mpunga, kwa
kutumia mbinu ya kilimo cha shadidi cha mpunga kwa kuwajengea uwezo wakulima,
Mradi wa kilimo cha shadidi umeanza miaka miwili iliopita kwa kuwapatia
wakulima mbegu sahihi zenye uzalishaji mkubwa.
Kati ya mbegu kumi zilizofanyiwa
utafiti, mbegu tano ndizo zilizofanikiwa kuchaguliwa na wakulima kutokana na
uzalishaji wake ambazo ni, Subang, Supa BC, TXD 88, TXD306, Supa India.
Comments