Hatua kali kuchukuliwa kwa waharibifu wa vivutio vya watalii Zanzibar.

Kamisheni ya Utalii Zanzibar  imesema itawachukulia hatua za kisheria  wananchi wanaofanya  hujuma  katika  fukwe za bahari kwa uchimbaji wa mchanga kwani kufanya hivyo ni kuondoa haiba  na  kutapelekea kushusha kipato katika sekta ya utalii.


Akizungumza  na Zanzibar 24 Afisa  Uhusiano  kamisheni ya utalii Mohammed Nassor Bajuni amesema  fukwe ni miongoni mwa  vivutio vya utalii kwa wageni wanaotembelea Zanzibar  lakini cha kusikitisha baadhi ya wananchi wanaoishi karibu na bahari  huzitumia vibaya fukwe kwa kuzifanyia uharibifu na kusababisha fukwe zile kuharibika na kupoteza ubora wake.

Hata hivyo Bajuni amesema  serikali za Wilaya na Mikoa kwa kushirikiana na Vikosi vya SMZ   bado  wananafasi kubwa ya  kuzisimamia  na kuzifanyia ulinzi  kwa umakini mkubwa  fukwe  ili kuzinusuru na uharibifu huo  kwani   utalii wa zanzibar unategemea fukwe katika mapato yake.

Amesema  uharibifu huo umekuja mara baada ya   serikali kuzuiya uchimbaji wa mchanga   na wananchi kuhamia  katika fukwe za bahari hivyo ametoa wito kwa wananchi kuwacha tabia ya uharibifu na badala yake kuzilinda  kwani faida yake ni kubwa katika taifa  na hata wao wenyewe.

Sekta ya utalii Zanzibar  inavivutio vingi ambavyo huwavutia wageni wanaotembelea Zanzibar  miongoni mwao ni  fukwe,majengo ya kihistoria,mapango,mji mkongwe na  misitu ya asili pamoja na wanyama pori.
chanzo: zanzibar24.

Comments