
Tukio hilo la mauaji ya watu 17 wa familia moja lilifanywa mwaka
2010 na Sura Bukaba Sura maarufu kwa jina la Phinias Yona au Epoda
mwenye miaka 35, mkazi wa wilayani Butiama mkoani Mara ambaye
amefikishwa katika mahakama ya Wilaya ya Musoma mkoani Mara mbele ya
hakimu Richard Maganga.
Akisomewa mashitaka yake ya mauaji ya watu 17 , Mwendesha Mashitaka
wa Polisi Jonas Kaijage, aliiambia mahakama kuwa mtuhumiwa akiwa na
wenzake wapatao 15, ambao wote wakazi wa wilayani humo, walitenda kosa
hilo Februari 16 mwaka 2010 majira ya usiku katika eneo la Mugaranjabo,
nje kidogo ya mji wa Musoma.
Kaijage alisema baada ya kutekeleza mauaji mtuhumiwa huyo
alitoroka, na wenzake 15 walikamatwa na kufikishwa mahakamani hapo
ambapo kati yao wanane walikwishafariki dunia wakiwa mahabusu.
Aidha Kaijage amesema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa Julai 18 mwaka
huu, kwa kesi nyingine ya unyang’anyi wa kutumia silaha katika eneo la
Rwamulimi mjini Musoma.
Alisema katika tukio hilo la unyang’anyi wa kutumia silaha,
mtuhumiwa huyo alivamia nyumbani kwa mwananchi mmoja na kuvunja nyumba
kwa kutumia nondo na kufanikiwa kuiba Sh 500,000,ndipo polisi
walifanikiwa kumkamata na kumtambua kuwa alishiriki katika tukio la
mauaji ya watu hao 17 lililotokea mwaka 2010.
Baada ya kusomewa mashitaka yake mtuhumiwa huyo hakutakiwa kujibu
chochote kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kisheria kusilikiza
kesi za mauaji na Hakimu Karimu Moshi aliahirisha kesi hiyo hadi Agosti 7
mwaka huu, itakapotajwa tena mahakamani hapo na kuunganishwa na
washitakiwa wengine waliosalia.
chanzo: zanzibar24.
Comments