Ushauri huo ulitolewa jana na Rais wa Chama cha Watu wenye Himofilia
Tanzania, Richard Minja wakati akitoa hotuba ya makaribisho katika
semina kwa waganga wa tiba asili na mbadala wa jijini Dar es Salaam
iliyofanyika jijini humo.
Alisema wagonjwa wengi wa himofilia wamekosa
tiba stahili na kusababisha athari kubwa hata wengine kufa kutokana na
kutopewa maelekezo mazuri na waganga wa tiba asili na mbadala wanapofika
kwao kupata matibabu.
“Tumewaita waganga wa tiba asili kupata semina kuhusu himofilia ili
waufahamu vizuri ugonjwa huu na wasaidie kuwapa rufaa wagonjwa maana
ugonjwa huu ni wa kisayansi na tiba stahiki inapatikana hospitalini,”
alisema Minja.
Alisema semina hiyo kwa waganga hao imeanzia Dar es
Salaam na itafikishwa nchini kote hasa vijijini ili kuwasaidia watoa
tiba hao kuuelewa ugonjwa huo na kushirikiana na vituo vya afya na
hospitali kuwaelekeza wagonjwa kupata tiba inayotakiwa kisayansi.
Kwa upande wake, Daktari bingwa wa magonjwa ya damu na Mkuu wa
Kitengo cha Magonjwa ya Damu Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dk Stella
Rwezaula, alisema wameelekeza semina kwa waganga wa tiba asili na
mbadala kwa kuwa Watanzania wengi wanakwenda kwao kuhitaji msaada.
Akielezea hali ya ugonjwa, Dk Rwezaula alisema kwa sasa nchini
wamesajili wagonjwa 110 pekee wa himofilia lakini zaidi ya Watanzania
5,400 wanaishi na ugonjwa huo na asilimia 97 hawajitambui kama wanao.
Aliwataka wananchi kuwa na utaratibu wa kupima afya ili kutambua kama
una ugonjwa huo au mwingine ili kuanza tiba na ushauri zaidi.
Dk
Rwezaula alisema ugonjwa huo unatokana na mtoto kuzaliwa akiwa
amepungukiwa na protini ya kugandisha damu ikiwa ataumia. Alisema
kutokana na upungufu huo, muathirika anapoumia, kupata ajali au mjamzito
wakati wa kujifungua hutoka damu nyingi na wakati mwingine kusababisha
vifo.
Alisema ingawa bado nchini utafiti wa kina haujafanywa kuhusu ugonjwa
huo, kwa sasa muathirika ataishi nao maisha lakini atapata tiba ya
kumpa ahueni kwa njia ya dawa (factor namba 8 na 9) na huchomwa kwa njia
ya sindano.
Naye Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Tiba Asili
Tanzania (Shivyatiata), Othuman Shem, aliwashukuru waandaaji wa semina
hiyo kwa kuwakumbuka waganga wa tiba asili na mbadala kupata semina hiyo
kuwezesha kuwapa rufaa wagonjwa wenye tatizo hilo pindi
watakapowafikia.
“Semina ni nzuri maana tumejua kuwa ni ugonjwa wa kisayansi wala si
mapepo au majini, hii itasaidia maana zaidi ya asilimia 60 ya Watanzania
wanakuja kwetu kwa tiba asili, tukiuelewa huu ugonjwa, mtu akija ni
rahisi kumshauri aende hospitali,” alisema Shem.
Alishauri semina hiyo
ifanyike nchi nzima ili waganga wengi wa tiba asili na mbadala waipate
kunusuru maisha ya Watanzania wenye himofilia.
chanzo:Habarileo.
Comments