Viwanda vya korosho kujengwa Mkuranga, Mtwara na Tunduru.

SERIKALI imo katika mchakato wa kuanzisha kiwanda cha korosho Mkuranga, Mtwara na Tunduru katika mwendelezo wa juhudi za kuwa na Tanzania ya uchumi wa kati na ya viwanda.

Tanzania inazalisha tani 260,000 za korosho kwa mwaka na sasa ina viwanda 12 vya ubanguaji. 

Akizungumza Dar es Salaam jana juu ya umuhimu wa kuacha utaratibu wa kusafirisha korosho ghafi zinazoyanufaisha mataifa mengine,
Mtafiti Kiongozi wa Programu ya Korosho Barani Afrika ambaye pia ni mjumbe wa Bodi ya Korosho Tanzania (CBT), Profesa Peter Masawe, amesema kiasi kikubwa cha thamani ya korosho kinapotea kwa kukosa umakini.

“Wabanguaji wa Tanzania wanachukua korosho karanga tu huku wakiacha kiasi kikubwa cha zao hilo ikiwemo maganda na mabibo ambayo yana thamani kubwa. Tutafute namna ya kuyaongezea thamani maganda na mabibo badala ya kutupa,” alisema.

Profesa Masawe alitolea mfano mataifa yanayonufaika na korosho za Tanzania ikiwemo India: “Tujiulize kwa nini mataifa ya India, China na Vietnam ndio walionunua korosho nyingi katika msimu uliopita kuliko wabanguaji wa ndani mbali ya kilo moja kufikia Sh 4,000 tena bila kujali gharama ya kusafirisha na kuhifadhi kwenye maghala wakifika kwao; maana yake wanapata faida kubwa.

“India, kwa mfano, wakibangua korosho ikitoka karanga wanaiuza kama chakula, vipande vya korosho wanatengenezea siagi, pasta na poda. “Kwenye maganda, wanatoa CNSL (Cashew Nut Shell Liquid) ambayo uzito wake inakua sawa sawa na korosho iliyotoka; yaani ikiwa ulipobangua ulipata kilo 10 ya korosho basi utapata kilo 10 ya CNSL ambayo inatumika kutengenezea brake linings, vipodozi, viuatilifu vya kuua mchwa na kilainishi katika mashine za ndege,” alisema Profesa Masawe.

Kwa upande wa mabibo, mtafiti huyo aliyebobea kwenye korosho alisema, juisi ya mabibo ina vitamin C mara 10 zaidi ya juisi ya nanasi na mara tano zaidi ya juisi ya machungwa, lakini pia mabibo yanatumika kutengeneza mvinyo na pombe kali aina ya Nipa. “Tukianzisha viwanda vitatu tutakuwa tumeiunga mkono serikali yetu katika azma ya kutufikisha katika uchumi wa viwanda.

Tujiulize ikiwa kiwanda kimoja kina uwezo wa kubangua tani 10,000 sisi tunazalisha tani zaidi ya 260,000 kwa mwaka na nina hakika msimu ujao tunaweza kufikia tani 300,000. “Maana yake tukiwa na viwanda zaidi ya 20 vinavyobangua tani 10,000 kila kimoja na kila kiwanda kikiwa na uwezo wa kutoa ajira zaidi ya 8,000, hizo ni ajira 80,000. “Kumbuka viwanda vingi havipo mjini, vipo maeneo zinapozalishwa korosho huko vijijini, kwanza tutapunguza msongamano mjini lakini pia tutaimarisha elimu, afya na miundombinu vijijini,” alisema.

Takwimu zinaonesha korosho ni zao linalokua kwa kasi katika ukanda huu wa kusini mwa jangwa la Sahara na msimu uliopita liliongoza kwa mauzo. Hata hivyo, Tanzania ina viwanda 12 vya kubangua korosho lakini changamoto ya kuuza korosho ghafi nje ya nchi haijapatiwa ufumbuzi.
chanzo:Habarileo.

Comments