Shida ya Maji Mwera kiungoni kuwa historia.

bumbwiniTatizo la maji linalowakabili wananchi wa kijiji cha Mwera Kiongoni, inatarajiwa kuwa historia baada ya wiki chache zijazo.

Matumaini ya kumalizika kwa kero hiyo yamekuja kufuatia Mwakilishi wa jimbo la Tunguu Simai Mohammed Said kukabidhi mipira sita ya kusambazia maji iliyogharimu shilingi 2,500,000.

Kwa miaka mingi, wananchi wa eneo hilo lenye historia kubwa kwa kuwa ndiko alikozaliwa Rais wa kwanza wa Zanzibar marehemu Abeid Amani Karume, wamekuwa wakitumia maji ya visima ambayo hayana uhakika wa usalama.


Akizungumza kwa niaba yake na Mbunge wa jimbo hilo Khalifa Salum Suleiman wakati wa makabidhiano hayo, Mwakilishi Simai alisema msaada huo ni miongoni mwa malengo yao ya kuwaondoshea wananchi shida mbalimbali zinazowakabili hatua kwa hatua.

Alisema baada ya kupokea taarifa kutoka uongozi wa wadi ya Ubago juu ya tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama, na sasa wanaanza harakati za kusogeza huduma hiyo karibu na wananchi.

Alifahamisha kuwa baada ya kutandikwa mipira hiyo ikiwa awamu ya kwanza, juhudi zitaendelea kufikisha maji kutoka Kwa kozi hadi Mkorogo, ili kuhakikisha viambo vyote vinapata maji kutoka masafa ya karibu.

Hata hivyo, aliwakumbusha wananchi wahakikishe kuwa mipira hiyo hawaitandiki karibu na hifadhi ya barabara, akisema iko katika mipango ya serikali kuitengeneza, kwani nayo ni miongoni mwa kero za muda mrefu zinazowakabili wanakijiji wa huko.

“Mbali na hapa, pia tuko katika juhudi za kuhakikisha maeneo yote ya jimbo letu la Tunguu yanaondokana na shida ya maji, hivyo tunaiomba Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) ituunge mkono,” alisema Simai.

Alitoa wito kwa vijana wa eneo hilo kujitokeza kwa wingi wakati wa kuchimba msingi utakaotandikwa mipira hiyo ili hatimaye maji yaweze kupatikana kirahisi.

Naye Diwani wa wadi ya Ubago Ussi Ali Mtumwa, alisema baada ya kupata mipira hiyo, sasa ni kazi tu, na kutaka wananchi wapange siku ya kuanza shughuli na kuimaliza haraka ili kutoa nafasi ya kuendelea na hatua nyengine.

Alisema mbali na changamoto ya maji, pia wanahitaji kujengewa barabara kwa kiwango cha lami, kwani kwa sasa iko katika hali mbaya.
chano: zanzibar24.

Comments