
hayo yameelezwa na MWENYEKITI wa Tume ya kurekebisha sheria Zanzibar Jaji Mshibe Ali Bakari, kwa
nyakati tofauti wakati akizungumza na masheha wa mkoa wa kaskazini
Pemba pamoja na wadau wengine alipokuwa akifungua mkutano wa
uwasilishaji wa rasimu za awali za sheria ya uharibifu wa mazao, sheria ya usajili wa nyaraka na urithi wa ardhi endelevu mkoani humo.
Alisema kwa sasa sheria hiyo inaendelea kufanyiwa mapitio na tume
yake kwa kuwashirikisha wadau mbali mbali na ndani ya sheria hiyo
vitakuwemo vifungu vinavyowagusa viongozi hao wa shehia iwapo watatoa
vibali kiholela.
Alisema wapo wafanyabiashara wanao yaharibu mazao kwa makusudi kwa
kuyachuma machanga au kuyaivishia kwa moto huku masheha wakishuhudia na
kuvifumbia macho vitendo hivyo jambo ambalo si sahihi na katika sheria
ijayo suala hilo litahesabika kama kosa.
Aidha Mwenyekiti huyo wa tume ya kurekebisha sheria, alisema hata
masheha kama wakijaribu kuwapa vibali vya kusafirishia wafanyabiashara
wenye tabia hiyo, nao sheria inawamulika hivyo lazima wajitenge na jambo
hilo.
“Sheria hii ambayo ni kongwe na sasa inafanyiwa
marekebisho, haitowagusa tu waharibifu wa mazao kama vile
wafanyabiashara wanaoingiza au kutoa nje ya Zanzibar mazao, hata masheha
wakitoa vibali kwa waharibifu nao watawajibika”,alifafanua.
Katika hatua nyengine Mwenyekiti huyo, aliitaja jamii kuendelea
kujenga utamaduni wa kusajili nyaraka zao pamoja na ardhi ili ziwe na
thamani kisheria.
Mapema Katibu wa Tume hiyo Asma Hamid Jidawi, alisema sheria ya
usajili wa ardhi endelevu, unalengo pia la kuondoa migogoro kwenye ardhi
za matumizi endelevu kama vile viwanja wa michezo, misikiti na
makanisa.
Baadhi ya masheha wa mkoa wa kaskazini Pemba, walisema kama sheria
hiyo itatekelezwa ipasavyo baada ya kupitishwa yaweza kuwa ni mwarubani
wa mazao kununuliwa yakiwa na uasili wake sokoni.
Sheha wa shehia Micheweni Dawa Juma Mshindo alisema Zanzibar
inazosheria nyingi na mzuri, ingawa changamoto huja kwenye utekelezaji
wake.
Akiswalisha mswada wa sheria ya usajili wa nyaraka mwanasheria kutoka
tume hiyo Mwita Khamis Haji, alisema sheria hiyo imeeleza aina mbili za
nyaraka zikiwemo za lazima na nyengine ambazo ni hiari.
“Nyaraka ya nyumba unayoishi au wa kiwanja cha nyumba
hizi ni lazima, ingawa zipo nyengine kama vile mikataba ya kijamii hizi
hulazimiki, ingawa faidi yake ukizisajili zipo”,alisema.
Tume ya Kurekebisha sheria Zanzibar chini ya Mwenyekiti wake jaji
Mshibe Ali Bakar imeshazifanyia marekebisho sheria 17 ikiwemo sheria ya
ushahidi, sheria ya wanyama, vileo na sheria ya usafirishaji baharini,
na kwa sasa wanaendelea na sheria za uharibifu wa mazao, nyaraka na
ardhi endelevu.
chanzo: zanzibar24.
Comments