Halmashauri Kigoma yapewa boti.

SHIRIKA la Maendeleo la Ubelgiji (BTC) limekabidhi kwa Halmashauri ya Wilaya Kigoma boti moja iendayo kasi kwa ajili ya utunzaji wa mazingira na kuzuia uvuvi haramu katika mwambao wa ziwa Tanganyika.

Akikabidhi nyaraka za boti hiyo kwa Mkuu wa Wilaya Kigoma, Samson Anga Meneja wa mradi wa uhifadhi mazingira na kuinua kipato kwa jamii wa BTC, Mayuma Cheyo alisema kuwa boti iliyogharimu kiasi cha shilingi milioni 19.5 itatumika kwa ajili ya shughuli za mradi katika eneo la mwambao wa Kaskazini wa ziwa Tanganyika.


Cheyo alisema katika utekelezaji wake boti hiyo itatumika kwa ajili ya kusafirisha watu wanaohusika na utekelezaji wa mradi, kufanya doria kuzuia uvuvi haramu na kulinda mazao ya samaki ambayo yamekuwa yakiharibiwa kwa kasi. 

Akizungumza baada ya kupokea boti hiyo Mkuu wa wilaya Kigoma, Samson Anga ametaka boti hiyo kutumiwa kwa shughuli zilizopangwa ili kuleta tija katika utekelezaji wa mradi huo.

Pamoja na hilo alisema boti hiyo itatumika pia kwa shughuli nyingine za maendeleo za utekelezaji wa shughuli za Halmashauri kwani kumekuwa na shida kufikia maeneo ya mwambao wa ziwa kutokana na kutokuwepo kwa nyenzo za usafiri kama hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya Kigoma, Hanji Godigodi alisema kuwa pamoja na kudhibiti uvuvi haramu na uharibifu wa mazingira katika vijijini vya mwambao wa ziwa Tanganyika lakini pia uwepo wa boti hiyo itasaidia katika ukusanyaji mapato wa leseni za uvuvi na mapato mbalimbali ya halmashauri.

Godigodi alisema kabla ya kupatikana kwa boti hiyo uvuvi haramu ulikuwa unafanyika kwa kiasi kikubwa kutokana na watendaji wa halmashauri kushindwa kuwafikia wavuvi wanaovua kwa kutumia nyavu haramu. 

Alisema walikuwa wakiwakimbia na kukimbilia kwenye kina kirefu cha maji, jambo ambalo halikuwa na ufanisi kwenye kudhibiti uvuvi haramu ambapo sasa boti hiyo itasaidia kukomesha uvuvi haramu.

Wenyeviti wa kamati za ulinzi za rasilimali za ziwa Tanganyika (BMU), Meko Mwangi kutoka Kijiji cha Mtanga na Mwema Hussein kutoka Kijiji cha Kigalye wamesema kuwa ulinzi waliokuwa wakiufanya bila kuwepo kwa nyenzo za kufanyia kazi ilikuwa kazi ngumu kwao na kwamba sasa udhibiti wa uvuvi haramu utafanikiwa kwa kiasi kikubwa.
chanzo:Habarileo.

Comments