Waumini wa kiislam Zanzibar wametakiwa kuzidisha umoja.

Imamu wa Marekani ambae pia ni Muhadhiri mkuu wa kimataifa Kassim Al-kan amewataka waumini wa dini ya kiislamu Zanzibar kuzidisha umoja wao katika kutekeleza neema za mwenyezi mungu hususan kipindi hichi cha kuelekea katika ibada ya funga Mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Akizungumza katika Kongamano la 9 ambapo kwa Zanzibar ni la  kwanza kufanyika  lililofanyika katika ukumbi wa baraza la wawakilishi la zamani  la kuukaribisha mwezi mtukufu wa ramadhani amesema katika kuelekea katika ibada ya funga waislamu hawana budi  kujiandaa  kwa mambo mema  na  kuzidisha unyenyekevu kwa Allah (S.W)
kwani ndio nguzo muhimu  pamoja na kusoma kitabu kitukufu Qur-ani.

Hata hivyo amesema waislamu wanajukumu kubwa kwa mwenyezi mungu katika kutekeleza ibada, hivyo umoja na mshikamano ndio ngao kubwa itakayo waunganisha na wasikubali nchi  yao ikawa na matabaka yatakayo sababisha mtafaruku na kupelekea  nchi ikawa katika machafuko.

Kwa upande wake Mufti mkuu wa Zanzibar Saleh Omar Kabi amewasisitiza waumini wa kiislamu kuwa na imani katika mwezi wa ramadhani kwa  kuwacha matendo machafu yatakayo batilisha funga zao badala yake kushiriki katika mambo mema ikiwemo kusoma qur-ani,kutoa sadaka pamoja na kuwa waja wema katika maisha yao yote.

Akitoa salam za serikali kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa baraza la Mapinduzi Dr.Ali Mohamed Shein Waziri wa Nch Ofisi ya Rais Katiba,Sheria,Utumishi wa umma na utawala bora Haroun Ali Suleiman amesema Serikali itakuwa bega kwa bega kwa wataoshiriki katika kuchafua mwezi mtukufu wa ramadhani kwa kuwachukulia hatua kali za kisheria ili kutoa fundisho wa kuheshimiwa mwezi huo.

Pia Haroun amesema kutokana  na umuhimu wa kongamano hilo la kuukaribisha mwezi mtukufu wa ramadhani serikali itahakikisha kila mwaka kongamano kama hilo linafanyika ili kuwajenga wananchi wa kiislamu.

Kongamano hilo la kuukaribisha mwezi mtukufu wa ramadhani limeandaliwa na Ofisi ya Mufti wa Zanzibar liliwakutanisha waislamu mbalimbali Zanzibar.

chanzo:Zanzibar24

Comments