Vikosi vya ulinzi vya Iraq katika hatari ya mashambulizi ya Marekani.

Katika hali ambayo harakati ya wananchi ya Hashdu sh-Sha'abi nchini Iraq katika kukabiliana na ugaidi inaendelea kupongezwa na viongozi, wananchi na hata katika fikra za walio wengi, wanamapambano wa harakati hiyo bado wanaendelea kushambuliwa na ndege za kijeshi za Marekani.

 Kitendo hicho kimefanya fikra za walio wengi kutoa radiamali wakisema kuwa, Marekani inakusudia kukwamisha juhudi za mapambano hayo dhidi ya ugaidi. 


Inaelezwa kuwa katika mwenendo wa mafanikio ya jeshi la Iraq dhidi ya magaidi, harakati ya Hashdu sh-Sha'abi imefanikiwa kukomboa mji wa al-Qairawan, magharibi mwa mji wa Mosul kutoka mikononi mwa genge la kigaidi na ukufurishaji la Daesh. 

Katika siku kadhaa zilizopita harakati hiyo ya wananchi ilianzisha operesheni za kuukomboa mji huo wa kistratijia ulio umbali wa kilomita 90 magharibi mwa Mosul katika mpaka wa Iraq na Syria, huku operesheni hizo zikizaa matunda Jumannde iliyopita.

 Baada ya miezi kadhaa ya vita na mapigano makali, jeshi la Iraq limezidi kusonga mbele huko magharibi mwa mji huo ambao ni makao makuu ya mkoa wa Nainawa (Nineveh) kaskazini mwa Iraq kwa ajili ya kuukomboa kikamilifu mji huo. 

Hii ni katika hali ambayo ukwamishaji mambo wa Marekani katika njia ya kupambana na ugaidi nchini Iraq, bado unaendelea kushududiwa.

Katika uwanja huo ndege za kivita za Marekani zimewalenga wanamapambano wa harakati ya wananchi ya Hashdu sh-Sha'abi waliopo katika maeneo ya mpakani ya nchi hiyo na Syria. 

Njama hizo za Marekani zinatekelezwa katika fremu ya siasa za chuki za Washington katika eneo kupitia misaada yake kwa nchi zinazopambana na ugaidi (yaani Iraq na Syria.) Marekani inatoa nara za kupambana na ugaidi katika hali ambayo kuna nyaraka mbalimbali zinazothibitisha kwamba makundi mengi ya kigaidi likiwemo genge hatari la Daesh (ISIS), yameanzishwa na kulelewa na idara za ujasusi za Marekani. 

Katika kitabu chake cha 'Machaguo Magumu' Hillary Clinton, waziri wa mambo ya nje wa zamani wa Marekani alikiri wazi kwa kusema: 'Ni sisi tuliounda kundi la ISIS.' Mwisho wa kunukuu.

 Katika uwanja huo makundi ya ukufurishaji na kigaidi kama vile Daesh (ISIS) yanatekeleza stratijia za Marekani katika eneo la Mashariki ya Kati hususan katika mataifa ya Syria, Iraq, Yemen na Libya. Katika mazingira hayo viongozi wa Marekani na kwa lengo la kufikia siasa zao za uhasama wanastafidi na harakati hizo za kigaidi katika njia ya kuharibu eneo la Mashariki ya Kati, kwa kuunda muungano eti wa kupambana na ugaidi.

Hata hivyo suala la kuzingatia ni hili kwamba, tangu kulipoundwa muungano huo bandia, utendajikazi wake umebainisha kuwa, malengo yake makuu sio kumaliza makundi ya kigaidi hususan Daesh (ISIS), kama inavyodaiwa na Washington, bali ni kuyaimarisha na kuyapa nguvu zaidi makundi hayo. 

Kwa msingi huo katika hatua ya mwisho ya mapambano dhidi ya ugaidi nchini Iraq, Marekani inafanya ukwamishaji mambo kwa kuwa serikali ya Trump imekusudia  kuzuia operesheni za kulimaliza kabisa kundi la Daesh bali inafanya juhudi za kuliimarisha zaidi kundi hilo la ukufurishaji nchini Iraq. 

Mbali na hayo ni kwamba hatua ya Marekani kushambulia maeneo ya askari wa harakati ya Hashdu sh-Sha'ab mjini Mosul inaibua maswali juu ya sababu kuu ya uadui wa Marekani kwa harakati hiyo. 

Harakati ya Hashdu sh-Sha'ab imelengwa na hujuma za kila upande za Marekani katika hali ambayo jeshi la Iraq limefikia mafanikio makubwa ya kukomboa maeneo mengi ya nchi hiyo yaliyokuwa chini ya udhibiti wa kundi la ukufurishaji na kigaidi la Daesh kupitia ushirikiano wa bega kwa bega na harakati hiyo.

 Itafahamika kuwa, mji wa Mosul ambao ulikuwa mji wa mwisho kwa wanachama wa kundi la Daesh kuonyesha nguvu zao, umekuwa pia wa mwisho kwa harakati ya Hashdu sh-Sha'ab kuonyesha nafasi yake muhimu katika mapambano yake dhidi ya magaidi hao. Kabla ya hapo Hashdu sh-Sha'ab ilikuwa na nafasi chanya katika ukombozi wa mikoa ya al-Anbar,  Diyalah na Salahd-Din kutoka mikononi mwa genge hilo. 

Hii ni katika hali ambayo vyombo vya habari nchini Iraq, vimeripoti habari ya kushushwa kwa helikopta za Marekani shehena za silaha kwa wanachama wa kundi la kigaidi la Daesh katika maeneo tofauti ya Iraq, suala ambalo linabainisha wazi kuwepo njama chafu za muungano huo wa Marekani nchini humo.
chanzo: parstoday.

Comments