Tanroads yatadharisha bomoabomoa nyingine.

Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa.WAKALA wa Barabara (Tanroads) Mkoa wa Dar es Salaam, umetoa siku 30 kwa wananchi waliojenga katika hifadhi ya barabara ya Morogoro kuanzia Kimara-Kiluvya kubomoa nyumba zao mara moja kupisha upanuzi wa barabara hiyo.

Meneja wa Tanroads wa Mkoa wa Dar es Salaam, Julius Ndyamukama, alisema notisi ya kubomoa majengo na ukuta katika barabara hiyo imetolewa kwa wahusika Mei 2, mwaka huu.


Alisema hakuna mwananchi yeyote aliyejenga kwenye hifadhi ya barabara atakayelipwa fidia na kuwataka kubomoa na kupisha ujenzi huo ndani ya siku 30 na wasipofanya hivyo taratibu za kisheria zitafuata.

“Hatua zitakazochukuliwa ni pamoja na kumbomolea mhusika na atalazimika kulipa gharama zote zitakazojitokeza katika utekelezaji wa zoezi hilo. Nyumba na mali zinazotakiwa kuondolewa zimewekewa alama X” alisema.

Mkuu wa Idara ya Mipango wa Tanroads Mkoa wa Dar es Salaam, Humphrey Kanyenye alisema ubomoaji huo umelenga upanuzi wa barabara hiyo na miradi mingine ukiwemo wa njia sita, barabara za mwendo wa haraka na sehemu za maegesho ya magari.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya wananchi ambao nyumba zao zimewekwa ‘X’ wameiomba Serikali kuzungumza nao kwanza na kuwapa utaratibu kuhusu fidia ili waendelee na ubomoaji.

Juma Abdul mkazi wa Kimara alisema wamesikia tetesi kwamba ukibomoa haulipwi kwa madai kwamba wapo eneo la barabara lakini wanashangazwa na hatua hiyo kwa kuwa wakati wanajenga serikali ilikuwa inaona na haikuchukua hatua.

Neema Joseph, mfanyabiashara wa Kimara alisema Serikali inapaswa kuangalia jinsi ya kuwasaidia wananchi hao. Naye Sikujua Athuman alisema yeye ni mzee aliyekaa eneo hilo kwa muda, lakini anashangaa kwa sasa kutakiwa kuvunja. Kwa upande wake, Joseph Mushi alisema kitendo cha kubomoa nyumba kimtarudisha kijijini kwa lazima.
chanzo:Habarileo.

Comments