
Alisema Taasisi zinazohusika na jukumu la kusimamia masuala hayo ni vyema zikahakikisha kwamba zinaharakisha mapendekezo hayo ili ile dhana ya Uhuru wa kupata Habari bila ya kuogopa inapatikana.
Balozi Seif Ali Iddi alitoa kauli hiyo wakati wa mazungumzo yake na Uongozi wa Baraza la Habari Tanzania { MCT } ulioongozwa na Katibu Mtendaji wake Bwana Kajubi Mukajanga aliokutana nao hapo Afisini kwake Mtaa wa Vuga Mjini Zanzibar.
Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeahidi kutoa kila aina ya msaada katika kuona Sekta hiyo muhimu kwa jamii inawajibika ipasavyo katika kuwapasha Habari Wananchi.
“ Habari ni Sekta muhimu inayotoa Taarifa na Elimu na kuwahusisha moja kwa moja Wananchi wa kawaida wakiwemo wakulima Vijijini ”. Alisema Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.
Balozi Seif kupitia Uongozi wa Baraza hilo la Habari Tanzania aliwakumbusha Wana Habari kuzingatia sheria na Maadili yao ya kazi katika kuandika Habari wanazozifanyia Utafiti wa kina ili zisaidie Wananchi kupata Habari za ukweli.
Akizungumzia changamoto ya Vitambulisho vya Kazi inayowakumba Wana Habari wanaotokea Tanzania Bara na kupangiwa kufanya kazi Zanzibar Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliahidi kulifuatilia kwa kina suala hilo ambalo bado halijawa kero kama yalivyo masuala mengine katika utendaji.
Alisema Waandishi wa Habari wanaotokea Tanzania Bara wanapaswa kuandaliwa utaratibu maalum wa kupata vibali vya kazi kwa vile wao hawahusiani na kuwa na Vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi katika kuomba kibali cha kufanya Kazi Zanzibar.
Balozi Seif alieleza kwamba mfumo unaotumika katika kuwapasha Habari Wananchi wa pande zote za Muungano hauna mipaka licha ya kwamba Sekta ya Habari sio Taasisi iliyomo ndani ya masuala ya Muungano.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliupongeza Uongozi wa Baraza la Habari Tanzania { MCT } kwa umakini wake wa kusimamia Sekta ya Habari Nchini Tanzania.
Mapema Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania { MCT } Bwana Kajubi Kukajanga alisema Kamati ya Maadili ya Bahara la Habari Tanzania imekuwa na utaratibu wa kufanya ziara za kusikiliza malalamiko yanayotolewa na Wananchi wanaoandikwa visivyostahiki katika Vyombo mbali mbali vya Habari.
Bwana Kajubi alisema Wajumbe wa Kamati hiyo kupitia ziara hizo hupata fursa za kushauri, kuelekeza pamoja na kuwaonya na wengine kuwachukuliwa hatua za kisheria Wana Habari wanaofanya makosa katika kuandika Habari chafu dhidi ya wananchi mbali mbali.
Alisema Viongozi hao pia wanajaribu kusaidia Wana Habari wanaotoka Tanzania Bara kuondokana na ukakasi wa kupata Vitambulisho vitakavyowapa fursa ya kufanyakazi kwa upana zaidi bila ya vikwazo.
Naye Mkuu wa Ofisi ya Baraza la Habari Tanzania { MCT } upande wa Zanzibar Bibi Shifaa Hassan alisema Mchakato wa Sera ya Habari Zanzibar umeanza tokea mwaka 2010 kwa mashirikiano baina ya Idara ya Habari Maelezo, Tume ya Utangazaji Zanzibar pamoja na baadhi ya Viongozi wa Taasisi za Serikali.
Bibi Shifaa alisema Zanzibar imekuwa tajiri katika masuala ya Historia ya Habari kutokana na kuanza mapema kwa Sekta hiyo ndani ya Ukanda mzima wa Afrika ya Mashariki.
Alisema Ofisi ya Baraza la Habari Tanzania upande wa Zanzibar ilianzishwa mwaka 2003 na kuanza na Mpango Maalum wa harakati za kutoa mafunzo kwa Wana Habari wachanga wa vyombo mbali mbali vya Habari wakiwemo pia wale waliomaliza masomo yao ya sekondari walioamua kujiunga na Tasnia hiyo.
Bibi Shifaa alieleza kwamba mpango huo ulikwenda sambamba na kutoa machapisho ya vitabu mbali mbali, kufanya utafiti kuhusu shirika la Habari Zanzibar mambo yaliyoibua kupatikana kwa Kitabu cha Historia ya masuala ya Habari Zanzibar kilichozinduliwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mwaka ulipita.
Viongozi wa Baraza la Habari Tanzania tayari wapo Visiwani Zanzibar kuhudhuria maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Habari Duniani inayofikia kilele chake ifikapo Tarehe 3 Mei ya kila mwaka ambapo Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi.
chanzo:zanzibar24.
Comments