Aliagiza pia halmashauri zote nchini zihakikishe zinajenga nyumba kwa
ajili ya watumishi wa afya hasa maeneo ya vijijini na kipaumbele
kitolewe kwa wakunga ambao mara nyingi ndio wanatoa huduma za dharura
kwa wanawake wajawazito na watoto.
Samia alitoa maagizo hayo mjini Dodoma katika kilele cha maadhimisho
ya Siku ya Wakunga Duniani, sherehe ambazo zimehudhuriwa na mamia ya
wakunga kutoka mikoa mbalimbali nchini.
Makamu wa Rais alisema kuwa halmashauri zikijenga nyumba karibu na
vituo vya kutolewa huduma za afya zitasaidia kupunguza matatizo ya mama
na watoto wanaotaka kupata huduma za dharura, ikilinganishwa na hali
ilivyo sasa ambapo baadhi ya watumishi wa afya hasa wakunga wanakaa
mbali na maeneo yao ya kazi hivyo utoaji wa huduma za dharura kuwa duni.
Alisema ni jambo la kusikitisha kuona Tanzania inarudi nyuma wakati
ilishapiga hatua katika jitihada za kutimiza lengo namba nne na lengo
namba tano la malengo ya milennia na kwamba hairidhishi kuona kuwa
wakati dunia imeshaanza utekelezaji wa ajenda ya maendeleo endelevu ya
mwaka 2030, Tanzania inaendelea kupoteza kinamama na watoto wengi.
Makamu wa Rais alisema bado Tanzania inapoteza kinamama 556 kutokana
na uzazi kwa kila vizazi hai 100,000 ukilinganisha na wanawake 432 kati
ya vizazi hai 100,000 miaka ya nyuma.
“Jambo hili halikubaliki ni lazima sote tushirikiane kuhakikisha
kuzaa haiwi adhabu kwa wanawake,” alisema Makamu wa Rais. Pia aliwataka
wakunga kuacha kauli chafu kwa mama mjamzito na kuongeza kuwa kesi za
wakunga zipelekwe kwenye mabaraza yao na kama ni kosa la jinai
akakumbane na sheria mahakamani.
Makamu wa Rais alisema mchango wa wakunga katika kutoa huduma za afya
ya uzazi ni mkubwa na wana jukumu kubwa la kuhakikisha lengo la
kuongeza kiwango cha kutumia uzazi wa mpango kinapanda kutoka asilimia
32 ya mwaka 2015/2016 hadi kufikia asilimia 45 mwaka 2020.
Rais wa Chama cha Wakunga Tanzania, Feddy Mwanga alitaka wakunga
wapatiwe makazi karibu na vituo vya afya kwani itasaidia huduma kuwepo
kwa saa 24. Kaulimbinu ya maadhimisho ya Siku ya Wakunga mwaka huu ni
“Wakunga, Akinamama na Familia ni washirika wa Kudumu.”
chanzo:Habarileo.
Comments