Sakata la vyeti feki, NECTA yafurika.

BARAZA la Mitihani Tanzania (NECTA) limeendelea kupokea umati wa watumishi wa umma waliojitokeza kukata rufaa na kuhakiki vyeti vyao ambao majina yao yalibainishwa kwenye orodha iliyotolewa na serikali ya watumishi walioghushi vyeti.

Gazeti hili lilishuhudia umati huo wa watumishi ukiwa umekusanyika katika ofisi hizo za Necta zilizopo Mikocheni jijini Dar es Salaam huku baadhi yao waliowahi wakipewa namba na kuingia ndani kuwasilisha vyeti na wengine wakisubiri nje kupangiwa utaratibu.


Akizungumza na gazeti la Habari leo jana, Ofisa Habari wa baraza hilo, John Nchimbi alikiri baraza hilo kupokea umati mkubwa wa watumishi hao wanaokata rufaa ambao wanaongezeka kila siku.

Nchimbi alisema kwa sasa kuna makundi matatu ya watumishi hao yakiwemo kundi la watumishi walioghushi vyeti, watumishi waliowasilisha vyeti visivyokamilika na watumishi wenye vyeti vyenye utata ambavyo cheti kimoja kinatumiwa na zaidi ya mtumishi mmoja.

“Kiutaratibu sisi Necta tunatakiwa kuwashughulikia watumishi waliopo kwenye orodha ya vyeti vyenye utata, tunamtaka mtumishi aliyekata rufaa awasilishe vyeti vyake halali kwetu tunampa namba na anaondoka zake,” alisema Nchimbi.

Hata hivyo, alifafanua kuwa pamoja na ukweli huo, makundi yote matatu yamejitokeza na kuwasilisha rufaa na malalamiko yao Necta jambo ambalo baraza hilo inabidi liwahudumie.

Alisema kiutaratibu watumishi ambao vyeti vyao havijakamilika, wanatakiwa kuwasilisha rufaa zao kwa waajiri wao na vielelezo baada ya hapo waajiri hao watawasilisha mbele ya baraza hilo rufaa hiyo iliyoambatana na vielelezo.

Kwa upande wa watumishi wenye vyeti vya kughushi wanapaswa kuwasilisha rufaa zao kwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala wa Bora ambaye ndiye atakayewasilisha rufaa hizo kwa baraza hilo la mitihani.

“Bahati mbaya kwa sasa wote wanakuja kwetu lakini tunawahudumia, tunajitahidi kuhakikisha kila mtu anapata haki yake, utaratibu mzijma ukikamilika kwa tarehe iliyotangazwa na Rais John Magufuli, tutapeleka idadi ya waliokata rufaa na matokeo kunakohusika,” alifafanua.

Baadhi ya watumishi waliojitokeza katika eneo hilo la Necta, walioomba kutotaja majina yao kwa usalama wao kikazi, walibainisha kuwa wameamua kukata rufaa kwa kuwa wana uhakika hawajaghushi vyeti vyao.

“Mimi nimeshangaa kuliona jina langu kwenye orodha ya walioghushi kwanza nimeshtuka sana, nimeambiwa vyeti vyangu vinatumiwa na watu wengine ambao hata siwajui, nimekuja hapa kuthibitisha kuwa mimi ndio mmiliki halali wa vyeti vyangu,” alisema mmoja wa watumishi hao aliyetambulisha kuwa anafanya kazi kwenye halmashauri.
Chanzo: Habari leo

Comments