Mvua hizo zinazoendelea kunyesha kwa takribani wiki tatu mfululizo
sasa, zimeacha athari kubwa katika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Dar es
Salaam, Pwani, Tanga na Zanzibar. Wabunge walioomba mwongozo baada ya
kumalizika Kipindi cha Maswali na Majibu ni Mbunge wa Korogwe Vijijini,
Stephen Ngonyani (CCM), Mbunge wa Vunjo James Mbatia (NCCR Mageuzi) na
wa Mlalo, Rashid Shangazi (CCM).
Ngonyani maarufu kama Profesa Majimarefu alisema kuna matatizo
makubwa ya mafuriko nchini.
“Kwenye mkoa wangu wa Tanga kumekuwa na
maafa, leo (jana) hii kuna watu 1,000 hawana chakula, mahali pa kuishi
na hawana msaada wowote, lakini serikali itawasaidiaje hawa watu wakati
kamati za afya zikiendelea na utaratibu,”alisema. Kwa upande wa Shangazi
alitaka shughuli za Bunge ziahirishwe ili wabunge wajadili kuhusu
mafuriko hayo.
“Sasa hivi katika mkoa wa Tanga kuna mafuriko makubwa sana. Jana
(juzi) yametokea maporomoko katika milima ya Usambara, eneo la barabara
za Lushoto- Arusha- Mombo , Pangani kwenda Tanga, Mombo kwenda Lushoto
na Kilindi kwenda Morogoro zote zilifungwa,”alisema.
Alisema Mkoa wa Tanga umegeuka kuwa kisiwa umepata athari kubwa hasa
Korogwe na kuiomba Serikali ilione hilo jambo ni la kimkakati na kwamba
Meneja wa Wakala wa Barabara (Tanroads) amezidiwa .
Alisema barabara hizo zimekuwa zikiunganisha mkoa huo na mikoa
mingine na kutaka Bunge lijadili angalau kwa muda mfupi.
Naye Mbatia
alisema hali ni tete kutokana na mafuriko yaliyojitokeza na kuomba utu
wa mwanadamu kuzingatiwa kama wawakilishi wa Watanzania kwa kutenga muda
wa angalau dakika 15 kujadili suala hilo.
“Tutenge muda wa dakika 15 ama 20 ili tujadili suala hili, ambayo ni
ya maafa tunaweza tukatoa majibu sahihi kwa wapiga kura wetu,
mwenyekitindio ombi langu kwa mujibu wa kanuni nilizozitumia,”alisema.
Akijibu miongozo hiyo, Mwenyekiti wa Bunge, Andrew Chenge, alisema
miongozo ya Mbatia na Shangazi imeangukia katika kanuni ya 47 (1) ambayo
inasomwa pamoja na kanuni ya 48. “Lakini kanuni ya 47(4) inampa Spika
mamlaka aridhike kama ombi hilo anaona jambo hilo kweli linahitaji
kusitisha shughuli zilizo mbele yetu ili kujadili hoja hizo za
dharura,”alisema.
Hata hivyo, alisema kwa hali anayoiona haoni kama suala hilo
linahitaji kujadiliwa sasa. “Ni kweli tukio hili limegusa maeneo mengi,
nawapa pole walioguswa kwa namna moja hata nyingine.
Naamini Serikali
iliyoko humu ndani itaitolea maelezo wakiangalia nchi nzima,”alisema na
kuongeza kuwa, anaamini Serikali italizungumzia vizuri kuliko kila
mbunge kujisemea katika eneo lake.
Kuhusu mwongozo wa Ngonyani, Chenge alisema kwa mujibu wa Kanuni ya
68 (7) ni lazima liwe tukio ama jambo ambalo limetokea mapema bungeni na
si nje. Polisi asombwa, afa Wakati wabunge wakitaka kujadiliwa kwa
athari za mvua zinazoendelea kunyesha, askari wa Jeshi la Polisi, Abbas
Anas Haji (55) amekufa maji baada ya kusombwa akiwa na pikipiki yake
aina ya Vespa wakati akipita eneo la barabara ya Fuoni Kibondemzungu
lililofunikwa na maji.
Tukio hilo limetokea jana majira ya saa 5:30
asubuhi wakati askari huyo akitokea kazini kwenda nyumbani kwake.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi Hassan Nassir Ali alisema
marehemu alikuwa ni mfanyakazi wa jeshi la polisi katika Kitengo cha
Picha, Makao Makuu ya Polisi upande wa Zanzibar.
Familia 150 zatangatanga Katika tukio jingine, zaidi ya familia 150
kisiwani Pemba zimekosa makazi na kulazimika kusitiriwa na ndugu na
jamaa baada ya nyumba zao kuathirika vibaya na mvua kubwa iliyonyesha
kwa siku tatu mfululizo.
Timu ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar iliyotembelea mikoa
miwili Pemba na kujionea athari za mafuriko, imeelezea kufurahishwa na
mshikamano mkubwa uliooneshwa na wananchi katika kusaidiana bila ya
kujali itikadi za kisiasa.
Waziri asiye na Wizara Maalumu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,
Ali Juma Khatib alisema wananchi wameonesha uzalendo wa hali ya juu
ambao watu wote walioathirika na mafuriko hayo wamehifadhiwa na kuishi
kwa ndugu na jamaa.
Aidha, Khatib waliwataka wananchi walioathirika na mafuriko hayo
wasirudi tena katika maeneo yao hayo ambayo athari zake bado zipo.
Ameahidi kusaidia na kutoa mifuko ya saruji 50 kwa familia za wilaya ya
Mkoani ili zikarabati nyumba zao.
Tanga-Arusha yafunguka Aidha, mkoani Tanga ambako miundombinu ya
barabara ilisababisha kukusekana kwa usafiri kati ya mkoa wa Tanga na
mikoa jirani ya Kilimanjaro na Arusha, hali imetajwa kurejea katika hali
yake ya kawaida.
Mkuu wa Wilaya ya Korogwe, Robert Gabriel akizungumza jana katika
mahojiano kwa njia ya simu alisema kiasi cha mvua inayonyesha kimeanza
kupungua ingawa ipo hali ya mawingu mazito katika baadhi ya maeneo.
Naye Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga, Benedict Wakulyamba
akizungumzia hali ya usalama kuhusu kifusi kilichoanguka na kufunga
sehemu ya eneo la barabara kuu inayounganisha miji ya Soni na Lushoto
alisema anaelekea eneo la tukio na kwamba atatoa taarifa.
Aidha, kuhusu mawasiliano ya barabara ya Tanga - Pangani alisema kwa
sasa watumiaji wa barabara hiyo wanapita katika njia mbili mbadala
ikiwemo ya Pongwe - Kirare jijini Tanga pamoja na ile ya Muheza- Misozwe
- Pangani ya wilayani Muheza wakati huu ambapo Tanroads wanafanya
jitihada za kutengeneza njia ya mchepuko katika eneo la daraja la Neema
lililopo kwenye barabara kuu ya Tanga- Pangani.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Tanga, Thobias Mwilapwa ameuagiza
uongozi wa Jiji la Tanga kuacha kufanya kazi kwa mazoea badala yake
wajitahidi kufanya utafiti wa maeneo ya ujenzi wa miundombinu ya
barabara na madaraja nyakati za msimu wa mvua badala ya kiangazi ili
kupata picha ya mahitaji halisi ya ujenzi tofauti na inavyofanyika sasa.
Ametoa maagizo hayo kwa nyakati tofauti jana alipozungumza katika
mahojiano na HabariLeo baada ya kutembelea baadhi ya mitaa ya jijini
Tanga iliyoathiriwa na mafuriko yaliyotokana na mvua isiyo ya kawaida
iliyonyesha mfululizo juzi kwa saa 24 na kusababisha maafa ikiwemo vifo
vya wakazi wawili.
Katika mji wa Tanga, mvua hizo ziliua watu wawili, nyumba 97
zilizingirwa maji pamoja na Soko maarufu la vyakula la Magandini na
kusababisha mali zote kupotea, nyingine 36 zilibomoka kabisa, moja
kutitia, nyingine kuteketea kwa ajali ya moto uliotokana na hitilafu ya
umeme ambapo kaya 59 zenye wakazi zaidi ya 200 walioathirika
walihifadhiwa katika kambi zilizopo kwenye shule ya msingi ya
Chumbageni, Kwakaheza, Magaoni, Mafuriko na Sekondari ya Hotten.
Mvua za kihistoria Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) hivi
karibuni ilitoa taarifa inayoonesha kuwa, mvua zinazoendelea kunyesha
katika maeneo mbalimbali mkoani Tanga zimefikia kiwango cha juu ambacho
hakikuwahi kurekodiwa tangu mwaka 1949, sawa na takribani miaka 68
iliyopita.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Utafiti wa mamlaka hiyo, Dk Ladislauds
Chang’a, mvua iliyonyesha kwa saa 24 Mei 9 mwaka huu mkoani Tanga ni ya
milimita 316, kiwango ambacho hakijarekodiwa kwa miaka mingi.
Aliongeza kuwa, hawajafanya tathimini, lakini mwaka 2014 kulikuwa na
kiwango kikubwa zaidi baada ya kunyesha mvua ya milimita 138 ndani ya
saa 24 na kwamba kiwango cha juu kwa historia ya kituo cha Dar es Salaam
ni mwaka 1953 iliponyesha mvua ya kiwango cha milimita 167.4.
Alisema
mvua za sasa zinatarajiwa kuendelea hadi mwishoni mwa mwezi huu.
Imeandikwa na Maulid Ahmed (Dodoma), Anna Makange (Tanga) na Khatibu Suleiman (Zanzibar).
chanzo:Habrileo.
Comments