LAPF watamba wapo salama dhidi ya vyeti feki.

Jengo la LAPFMFUKO wa Pensheni wa LAPF haujatikiswa na sekeseke hivi karibuni la kuondolewa wafanyakazi hewa na wenye vyeti feki nchini tofauti na watoa huduma za kijamii wengine ambao wamepata mushtuko kutokana na kuondolewa kwao.

Tangu serikali imeanza kuwaondoa wafanyakazi hewa na wenye vyeti feki kwenye serikali za mitaa na katika mashirika ya umma na wizara baadhi, mfuko huo haujatikisika kutokana na mfumo mzuri wa utoaji huduma zake.


“Tupo salama, tumeomba serikali ituletee orodha ya majina ya watumishi wa serikali ambao wameingizwa kwenye orodha ya wafanyakazi hewa na wenye vyeti feki, sera za mfuko wetu zipo wazi na ndio mfuko wetu upo imara, ndio umetoa mikopo kwa ajili ya watu mbalimbali kujiendeleza kielimu na tunatoa mikopo isiyozidi asilimia 75 ya michango, hata kama wakiondolewa kazini wanaweza kuwa na njia mbadala kulipa deni hilo,” alisema Kaimu Meneja wa Matekelezo, Voctor Kikoti.

Hadi Aprili mwaka huu, mfuko umetumia zaidi ya Sh bilioni 2.4 kwa ajili ya kusaidia wanachama 1,438 wanaotaka kujiendeleza kielimu katika ngazi mbalimbali ndani na nje ya nchi. “Mfuko pia umetoa zaidi ya Sh bilioni 9.54 kwa ajili ya wanachama 11,744 waliojiunga na mfuko huo kwa ajili ya mafao ya kujifungua,” alisema Kikoti.

Meneja wa Masoko na Mawasilianowa LAPF, James Mlowe alisema mfuko huo unaongoza katika kufanya vizuri ukilinganisha na mifuko mingine na umepata maendeleo makubwa tangu kuanzishwa kwake na hasa tangu Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA), ilipofungua milango mifuko yote kutafuta wanachama kutoka sekta mbalimbali.

Mlowe alisema, kabla ya mfumo huo wa SSRA, ilikuwa ikishughulikana na wafanyakazi wa serikali za mitaa tu, mara baada ya kufungua milango hiyo, imeingia kutafuta wanachama kwenye mashirika ya umma, sekta binafsi na sasa imeingia serikali kuu.

Alisema mfuko huo wa LAPF hadi Aprili Mwaka huu una wanachama 172,000, licha ya uhaba wa ajira katika mwaka uliopita, mfuko huo ulifaulu kuwasajili wanachama wapya 16,839.

Mfuko huo uliosajiliwa mwaka 1944 na baadaye kuundwa upya nchi ya sheria Namb 9 ya 2006 inatoa mafao mbalimbali yakiwa ya penseni ya uzee, ulemavu, warithi pamoja na uzazi, mazishi na mikopo ya elimu. Mengine ni mafao ya kustaafu na kujitoa pamoja na ndoa, uhamiaji au kutokuwa na ajira na ugonjwa.
chanzo:Habarileo.

Comments