Jenerali Dehqan: Tuna uwezo wa kuuza nje makombora na kuongeza kiwango cha uundaji silaha kwa asilimia 100.

Waziri wa Ulinzi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Brigedia Jenerali Hussein Dehqan amesema, mbali na Iran kujitosheleza kwa mahitaji ya ndani ina uwezo pia wa kusafirisha na kuuza nje ya nchi makombora yanayoundwa hapa nchini.

Brigedia Jenerali Dehqan amesisitiza kuwa katika teknolojia ya uundaji makombora, hivi sasa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imefikia kiwango cha uwezo wa kuunda kombora la masafa yoyote inayotaka, lenye nguvu ya kusababisha kiwango chochote cha uharibifu inachokusudia na umakini wa juu kabisa wa kulenga shabaha. 


Ameongeza kuwa mafanikio ya kiulinzi iliyopata Iran ni ya malengo ya kujihami tu kwa ajili ya kukabiliana na maadui.

Waziri wa Ulinzi wa Iran aidha amebainisha kuwa bei na ubora wa zana za kijeshi za Iran ni wa namna ambayo licha ya vikwazo vya kidhalimu ambavyo madola ya Magharibi yaliliwekea taifa hili, zana hizo za ulinzi zinazozalishwa hapa nchini zinasafirishwa na kuuzwa katika nchi kubwa kubwa duniani.
 
Brigedia Jenerali Dehqan ameashiria pia kuongezeka katika kipindi cha miaka ya karibuni kwa kiwango cha asilimia 100 silaha zinazotengezwa nchini na kueleza kuwa, leo hii Wizara ya Ulinzi ya Iran ina uwezo wa kuzalisha silaha na zana zote zinazohitajiwa na vikosi vya nchi kavu vya jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.

Waziri wa Ulinzi wa Iran ameongeza kuwa maendeleo yaliyopatikana na hatua zilizopigwa ni matunda ya jitihada za vijana wenye hima kubwa na moyo wa kujitolea wa taifa adhimu la Iran.
chanzo: parstoday.

Comments