Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto imefanikiwa kuwarejesha skuli watoto 5,067 na kuwapeleka elimu mbadala.
Aliyasema
hayo wakati akiwasilisha ripoti ya ajira za watoto na walio katika mazingira
magumu kwa Kamati ya Maendeleo ya Wanawake,
Habari na Utalii ya Baraza la
Wawakilishi, katika ukumbi wa Wizara ya Katiba na Sheria Pemba.
Amesema
kuwa, kati ya watoto hao, jumla ya watoto 1,188 wametolewa katika ajira za
watoto wakiwemo wanawake 479 na wanaume 709, ambapo jumla ya 3,879 walikuwa
katika hatari ya kuingia katika ajira za watoto.
Ameeleza
kuwa, watoto hao 5,067 walifikiwa na mradi wa ‘Fighting Against Child Labour in
Zanzibar’ ambapo serikali ikishirikiana na save the Children chini ya ufadhili
wa Jumuiya ya Ulaya (EU), ambao ulitekelezwa kwa muda wa miaka mitatu, ukiwa na
lengo la kupunguza ajira za watoto Zanzibar kwa shehia 50.
Kwa upande
wake Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya Wanawake, Habari na Utalii ya Baraza
la Wawakilishi Ali Suleiman Ali, amewataka wazazi kuwapeleka watoto skuli, ili
kuweza kupata elimu itakayoweza kuwasaidia katika maisha yao baadae.
Nae Sheha wa shehia ya Micheweni Juma Dawa
Mshindo alisema kuwa, kwa sasa hali inaridhisha ukilinganisha na kipindi cha
nyuma, kwani watoto wanakwenda skuli na wanaporudi ndio wanakwenda kubanja kokoto.
Katika ziara
hiyo pia iliwasilishwa ripoti ya utendaji wa Idara ya Ajira kwa kipindi cha
Januari hadi Machi mwaka huu na Mkurugenzi wa Ajira Ameir Ali Ameir na kusema
kuwa, Idara imesajili vijana 731, ambapo jumla ya vijana 170 wamepata fursa ya
ajira nje ya nchi.
Comments