Waziri :Taasisi za umma lazima zijiunge NHIF.

SERIKALI imesema ni lazima kwa taasisi na mashirika ya umma kujiunga na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF).

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu ametoa agizo hilo bungeni wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Ulanga, Goodluck Mlinga (CCM).


Waziri Ummy amesema suala la mashirika na taasisi za umma kujiunga na NHIF halina mjadala, ni suala la lazima na hivyo ni vema taasisi zote na mashirika ya umma yakajiunga na mfuko huo haraka iwezekanavyo.

Amesema, kuna mashirika na taasisi za serikali ambazo hawajajiunga na NHIF, hivyo serikali inaendelea na mazungumzo na taasisi hizo ili kuhakikisha kuwa wanafanya hivyo mara moja.

Akijibu swali la msingi la mbunge huyo aliyehoji ni taasisi na mashirika ya umma mangapi yamejiunga na NHIF, Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Hamisi Kigwangalla alisema hadi kufikia Machi, mwaka huu idadi ya wanachama katika mfuko huo ni 792,987 kutoka wanachama 474,760 mwaka 2012.

Alisema tangu kuanzishwa kwake mwaka 2001, mfuko huo umefanya maboresho mbalimbali ya vitita vya mafao na namna ya kuchangia kwa makundi mbalimbali ya jamii.

"Maboresho haya yamewezesha kwa kiasi kikubwa kuongeza idadi ya wanachama walio katika mfumo huu wa bima ya afya nchini na kufanya wanufaika kufikia asilimia nane. Hadi kufikia Desemba 31 mwaka jana idara za serikali, taasisi na mashirika ya umma zinazotumia huduma za bima ya afya za NHIF zimefikia 307. Idadi hii imetokana na jitihada za makusudi za kutoa elimu kuhusu umuhimu wa kuwa na bima ya afya kwa watumishi wa umma," amesema.

Amesema mashirika, taasisi na idara za serikali ambayo hayajajiunga na mfuko huo yapo 23 yakiwemo Mamlaka ya Mapato (TRA), Benki Kuu (BoT), Shirika la Umeme (Tanesco), Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari(TPA), PSPF, LAPF, PPF, Ewura, NCA na GEPF.
 chanzo:Habarileo.

Comments