Kwa mujibu wa wamiliki hao, wanahitaji rasimu ya kanuni hiyo itambue
na kutenganisha makosa yanayofanywa na dereva na yale yanayomhusu
mmiliki, lakini pia iandikwe kwa lugha ya Kiswahili.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya
Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (Sumatra), Gilliard Ngewe
alisema usitishwaji wa mgomo huo umekuja baada ya kuwepo kwa majadiliano
ya muda mrefu kati ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano,
Profesa Makame Mbarawa na wadau hao wa usafirishaji.
“Baada ya vyama hivyo kutangaza kuwepo kwa mgomo kuanzia kesho (leo),
waziri alikutana na wahusika hao kuanzia jana asubuhi na kujadiliana
kuhusu kanuni hizo akiwashirikisha pia Sumatra na wameafikiana mambo
mawili makubwa,” alibainisha Ngewe.
Alisema katika majadiliano na waziri, wamekubaliana kuwa ndani ya
siku 14 rasimu yote iandikwe kwa Kiswahili na wadau wa usafirishaji
kutoka vyama hivyo waipate na kutoa michango yao kwa ufasaha kwa
Kiswahili. Jambo la pili walilokubaliana ni kanuni hizo kutenganisha
makosa ya wamiliki wa mabasi na makosa yafanywayo na madereva.
Alisema kimsingi sheria inayowasimamia madereva ni ya usalama
barabarani, hivyo ina kanuni zake na sheria ya wamiliki ni ya leseni za
usafirishaji ya mwaka 1973 pamoja na marekebisho yote yaliyowahi
kutokea.
Alisema kilichotokea ni makosa ya dereva kutoelezwa katika rasimu ya
kanuni, hivyo kwa majadiliano hayo, katika rasimu ya kanuni hiyo
inatakiwa kuonesha makosa yapi ya dereva na ya mmiliki wa mabasi na
wakati hayo yakitekelezwa, usafiri wa abiria na mizigo nchini unaendelea
kama kawaida.
Naye Makamu Mwenyekiti wa Taboa, Abdallah Kiongozi alisema kiongozi
wa vyama hivyo vya usafirishaji kwa pamoja wamekubaliana kusitisha mgomo
na usafiri utaendelea kama kawaida.
chanzo:habarileo.
Comments