Waislamu Nigeria wafufua maandamano ya kushinikiza kuachiwa huru Sheikh Zakzaky.

Kwa mara nyingine tena Waislamu nchini Nigeria wamefanya maandamano ya amani katika mji mkuu wa nchi hiyo, kushinikiza kuachiwa huru mwanazuoni wa Kiislamu nchini humo, Sheikh Ibrahim Zakzaky.

Wafuasi wa Harakati ya Kiislamu Nigeria wakiwa pamoja na wanafunzi na wanachuo wa taasisi mbali mbali za elimu nchini humo, waliandamana kwa amani na kisha kupiga kambi nje ya manjengo ya Bunge katika mji mkuu Abuja, ambapo wamekabidhi waraka wa matakwa yao kwa afisa mmoja wa Bunge.

Waandamanaji hao wamesema kuwa harakati hiyo ni ya amani na haina historia ya kutumia mabavu wala silaha. Wamesema Sheikh Zakzaky amekuwa akihubiri amani kwa zaidi ya miongo mitatu na hivyo tuhuma dhidi yake eti anachochea ghasia nchini humo hazina msingi.
Licha ya muhula uliotolewa na Mahakama ya Federali kwa ajili ya kuachiliwa huru msomi na mwanaharakati huyo wa kidini kumalizika tarehe 16 Januari mwaka huu, lakini serikali haijatekeleza amri hiyo.
Kwa mujibu wa hukumu iliyotolewa tarehe Pili Disemba mwaka jana na mahakama hiyo, kitendo cha kuendelea kushikiliwa na serikali ya nchi hiyo Sheikh Zakzaky, mke na wanaharakati wengine wa Kishia ni kinyume cha sheria.
Shakhsia huyo ambaye hali yake ya afya inaripotiwa kuwa mbaya alikamatwa pamoja na mkewe baada ya askari wa jeshi la Nigeria kuvamia Husainiyyah ya Baqiyatullah katika mji wa Zaria, jimbo la Kaduna Disemba 13 mwaka 2015, na kuwaua shahidi mamia ya Waislamu wakiwemo watoto watatu wa kiume wa Sheikh Zakzaky.
chanzo:parstoday.

Comments