Wacharazwa kwa kukamata mtuhumiwa wa bangi.

BangiKAIMU Mtendaji wa Kijiji cha Imenya, James Martin na Mtendaji wa Kata ya Lugubu wilayani hapa, Leos Dotto wamecharazwa bakora na kundi la watu wa familia moja baada ya kumkamata mmojawao akiwa na dawa za kulevya aina ya bangi katika Kijiji cha Imenya, Kata ya Lugubu.

Akizungumza jana, Mtendaji wa Kata ya Lugubu, Dotto alisema hayo yalitokea wakati yeye na mgambo watatu, Zengo Salum, Juma Gaston na Luziga Kashindye walipokwenda kijijini hapo kufanya sensa ya mifugo kwa baadhi ya wafugaji waliokuwa wamegoma kuhesabu mifugo yao.

Alisema wakiwa njiani wanakwenda, walipata taarifa kuwa kuna kaya moja imeanika dawa za kulevya aina ya bangi kwenye kichanja cha miti huku nyingine zikiwa zimelimwa katika mashamba ya familia hiyo.

Dotto alisema baada ya taarifa hiyo, walikwenda hadi kwenye mji huo wa Sweya Nhunyula ambako walikuta bangi zaidi ya gunia moja ikiwa imeanikwa.

Na walipokwenda shambani, walikuta michezo zaidi ya 103 iliyolimwa katikati ya shamba huku ikiwa imezungukwa na mazao ya mahindi.

Alisema baada ya hapo, alipiga picha bangi hiyo huku wahusika wakiwa wameshika mimea hiyo na baadaye walirudi nyumbani kwa watuhumiwa huku akipiga simu Kituo cha Polisi Igunga.

Alifafanua kuwa, wakati yeye na wenzake wakiwasubiri polisi, ghafla alijitokeza mama wa nyumba hiyo, Yunge Zengo na kutangaza kutokuwa tayari kwenda polisi, ndipo Kaimu Mwenyekiti wa kitongoji hicho, Gambo Sweya ambaye ni mtoto wa Sweya Nhunyula alipoungana na nduguze kuwashambulia kwa fimbo watendaji, kitendo kilichowafanya mgambo na mtendaji wa kijiji kukimbia.

Anasema waliacha kumpiga baada ya kumwamuru akabidhi kitabu alichokuwa ameandika majina yao pamoja na sahihi zao. Aliruhusiwa kuondoka na pikipiki, bila kubeba dawa hizo.

Siku iliyofuata polisi walifika kijijini hapo na kukuta familia yote ikiwa imehama huku bangi iliyong’olewa shambani ikiwa imefichwa.

Mtendaji huyo na Mtendaji wa Kijiji, James Martin wameripoti tukio Polisi, ambayo kupitia kwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Hamisi Selemani imekiri kupata taarifa za tukio hilo.
chanzo:Habarileo.

Comments