
Hayo yalielezwa na Mratibu Mkaazi wa Umoja wa
Mataifa nchini Tanzania ambaye pia, ni Mwakilishi Mkaazi wa Shrika la
Maendeleo la Umoja wa Mataifa UNDP Alvero Rodriguez akiwa amefuatana na
viongozi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa wanaofanya kazi zao hapa
Zanzibar ambao wapo hapa nchini kwa mkutano maalum wa kila mwaka
unaofanywa na Umoja huo.
Mapema akitoa maelezo yake Mratibu huyo Mkaazi wa UN nchini Tanzania
ambaye alifuatana na Wawakilishi Wakaazi wa Mashirika ya UN wanaofanya
kazi zao hapa Tanzania alitoa pongezi kwa Dk. Shein kwa Serikali
anayoiongoza kwa kusimamia vyema miradi ya maendeleo na kuahidi
kuendelea kuunga mkono juhudi hizo.
Rodriguez alisema kuwa UN inathamini sana uhusiano na ushirikiano
uliopo kati yake na Tanzania ikiwemo Zanzibar, hivyo basi ni vyema hatua
hizo zikaendelezwa kwa manufaa ya nchi na wananchi wake wote.
Katika maelezo yake Rodriguez alieleza kuwa UN imeamua kwa makusudi
kuendelea kuunga mkono sekta za maendeleo zikiwemo elimu, afya, kilimo,
mazingira, athari za tabia nchi, kupambana na umasikini pampja na
unyanyasaji wa kijinsia kwa akina mama na watoto, changamoto ya ajira,
na nyenginezo.
Aidha, alisema kuwa UN iko tayari kuendelea kuunga mkono seta hizo
hasa ikizingatiwa kuwepo kwa madaliko makubwa ya kiuchumi duniani hatua
ambayo inatoa nafasi kwa Umoja huo kuongeza nguvu kwa Mashirika yake
kuendelea kusaidia nchi kama Tanzania ikiwemo Zanzibar.
Sambamba na hayo, kiongozi huyo wa UN nchini Tanzania alieleza hatua
zinazoendelea katika kuiunga mkono Zanzibar katika hatua zake za Kukuza
Uchumi na Kupambana na Umasikini na kutekeleza Dira 2020.
Nao ujumbe huo wa UN nchini Tanzania, kupitia Mashirika yake yalitoa
pongezi kwa Dk. Shein kutokana na uongozi wake katika kuendeleza miradi
ya maendeleo inayosimamiwa na mashirika hayo huku wakiahidi kuendelea
kumuunga mkono.
Nae Rais Dk. Ali Mohamed Shein kwa upande wake alitoa pongezi kwa
Umoja wa Mataifa kupitia mashirika yake kwa mashirikiano makubwa
inayoyatoa kwa Zanzibar na Tanzania kwa jumla.
Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza changamoto mbali mbali zilizopo
katika sekta za maendeleo ikiwemo elimu, afya, ajira, unyanyasaji wa
wanawake na watoto, athari za tabia na mambo mengineyo.
Hata hivyo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuueleza ujumbe huo wa UN
kuwa mbali ya changamoto hizo Zanzibar haikufunga mikono na imekuwa
ikichukua juhudi za makususdi katika kuhakikisha changamoto hizo
zinapatiwa ufumbuzi kwa mashirikiano ya Mashirika hayo ya Umoja wa
Mataifa.
Dk. Shein alisema kuwa hatua mbali mbali zimekuwa zikichukuliwa na
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha sekta ya elimu kwa
kuendelea na ujenzi wa skuli mpya za Msingi na Sekondari, Vyuo Vikuu.
Aidha, alieleza namna Serikali ilivyoelekeza nguvu katika kilimo cha
umwagiliaji maji.
Pia, alieleza juhudi zinazochukuliwa katika kuimarisha sekta ya
afya,mafanikio yaliopatikana katika kupambana na Malaria, kupambana na
unyanyasaji wa akina mama na watoto na kueleza mikakati mipya iliyowekwa
na Serikali katika kupambana na kadhia hiyo hivi sasa.
Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa kuwepo kwa Ofisi za pamoja za Umoja wa
Mataifa hapa Zanzibar ‘One UN’ kumeweza kurahisisha kwa kiasi kkkubwa
ufanyaji kazi wa Mashirika hayo na kupelekea kufanya kazi kwa ufanisi
mkubwa zaidi.
Wakati huo huo, Dk. Shein alikutana na Mabalozi wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania waliokuja kumuaga Rais, ambapo akitoa
nasaha na maelekezo kwa Mabalozi hao, Dk. Shein alisema kuwa nchi zote
wanazokwenda kufanya kazi Mabalozi hao ni muhimu na kuwataka kutambua
kuwa katika ufanyaji kazi wao wajue kuwa Jamhuri ya Muungani wa Tanzania
ina pande mbili.
Alieleza haja ya kuimarisha uchumi wa kidiplomasia katika uwakilishi
wao katika nchi watakazozifanyia kazi na kusisitiza kuwa katika suala
zima la uchumi hivi sasa Tanzania imeweka kipaumbele sekta ya viwanda
hivyo, ni vyema wakaitangaza ikiwa ni pamoja na kuwashajiisha wawekezaji
kuja kuekeza hasa katika sekta ya viwanda.
Pamoja na hayo, alieleza haja kwa viongozi hao kuutangaza utalii wa
Tanzania ambapo kwa upande wa Zanzibar na Tanzania Bara sekta hiyo
imeendelea kupewa kipaumbele kutokana na mchango wake mkubwa wa uchumi
na pato la Taifa kwa ujumla.
Aidha, alisisitiza haja ya kuyashajiisha mashirika ya ndege kufanya
safari zao hapa Tanzania yakiwemo mashirika ya ndege ya India,
Ujerumani, Algeria na nchi nyenginezo huku akitilia mkazo umuhimu wa
kuwasaisia wanafunzi ambao wanasoma katika nchi wanazoenda kuzifanyia
kazi pale wanapokuwa na matatizo yao.
Nao Mabalozi hao walimshukuru Dk. Shein kwa nasaha na maelekezo yake
na kuahidi kuyazingatia na kufanya kazi hasa suala zima la uzalendo
katika Muungano.
Miongoni mwa Mabalozi hao ni Balozi Omar Yussuf Mzee anekwenda nchini
Algeria, Balozi Abdalla Saleh Posi anenkwenda nchini Ujerumani, Balozi
Baraka Luvanda anaekwenda India, Balozi Sylivester Ambukile anaekwenda
nchini Afrika Kusini, Balozi Daudi Massima anekwenda nchini Israil na
Balaozi Sylivester Massele Mabumba anaekwenda Umoja wa Visiwa vya
Comoro.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
chanzo: zanzibar24.
Comments