Mkurugenzi Mkuu wa Sumatra, Gilliard Ngewe alisema hayo wakati
akizindua mafunzo ya usalama kwa waendeshaji wa boti ndogo katika Wakala
wa Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) uliopo Mbegani wilayani Bagamoyo,
Mkoa wa Pwani.
Ngewe alisema kuanza kwa mafunzo ya usalama kwa waendesha boti ni
jambo muhimu litakalowezesha kuimarisha sekta ya uvuvi, lakini pia kutoa
ujuzi kwa mabaharia waliopo nchini.
Alisema ili kutekelezwa kwa sera ya Tanzania ya viwanda yapasa kuwepo
kwa mafunzo hayo ya usalama katika ukanda wa bahari na hata katika
maziwa, jambo litakalosaidia kuongezeka kwa ajira kwa vijana walio
wengi, lakini pia kuimarika kwa lishe na afya ya Watanzania.
Mkurugenzi Mkuu wa Sumatra alieleza kuwa kwa kuimarishwa kwa sekta ya
uvuvi, itasaidia Tanzania kusafirisha mazao ya samaki kutoka Bahari Kuu
hadi katika viwanda vyenye kuchakata samaki kama ambavyo nchi za nje
hufanya na kusaidia kuimarisha uchumi wa eneo lao.
Alisema mafunzo hayo pia yatasaidia vijana wa Kitanzania ambao ni
mabaharia kuingia katika meli kubwa, na kutokana na ujuzi watakaoupata
wataleta maendeleo nchini.
Awali, Mtendaji Mkuu wa FETA, Yahya Mgawe alisema sababu ya mafunzo
hayo inatokana na kuwepo kwa ajali nyingi za majini na wakati mwingine
kuhatarisha maisha ya walio wengi.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Mabaharia nchini, Frank Chuma alisema
mafunzo hayo yatasaidia kuinua hadhi ya mabaharia nchini kwa kuwa
walisahaulika na kuonekana wasioweza kupata ajira kutokana na wengi wao
kutokupita katika vyuo vinavyotambulika.
chanzo:Habarileo.
Comments