Rais wa Zanzibar Dk. Shein azungumza na Walimu Pemba.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itahakikisha inawajengea mazingira bora walimu yakiwemo maslahi yao sambamba na kutatua changamoto zilizopo katika sekta hiyo hatua kwa hatua.

Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mkutano na Waalimu wa Skuli za Sekondari kwa skuli za Mikoa yote miwili ya Pemba, huko katika ukumbi wa Fidel Castro, Mkoa wa Kusini Pemba.


Katika maelezo yake Dk. Shein alieleza kuwa changamoto nyingi ambazo zimekuwa zikiikabili sekta ya elimu tayari zimeshaanza kufanyiwa kazi na Serikali anayoiongoza hatua ambayo ni uthibitisho kwamba Serikali ina dhamira ya dhati katika kuimarisha sekta ya elimu pamoja na sekta nyengine za maendeleo hapa nchini.

Alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kutatua changamoto hizo kwa mujibu wa fedha zilizopo Serikalini ili kufanikisha utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo ya Elimu 2016/2020, Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2015-2020, Mpango wa MKUZA III  pamoja na mipango mengine ya maendeleo ya Kitaifa na Kimataifa.

Dk. Shein alisisitiza kuwa Serikali itaweka kipaumbele maalum katika kuimarisha mazingira ya kufanya kazi walimu ili yawe bora zaidi ambapo itahakikisha muundo wa utumishi wa Wizara ya Elimu unafanyiwa kazi ili kila mfanyakazi wakiwemo walimu wapate stahiki zao kwa mujibu wa sifa za kitaaluma, uzoefu na dhamana zao.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa waalimu wote wa Sekondari hapa Zanzibar kwa kupelekea kuongezeka kiwango cha ufaulu wa wanafunzi wa  Kidato cha Pili, Kidato cha Nne na cha Sita .

Dk. Shein pia, alitoa pongezi kwa dhati waalimu hao kwa matokeo ya mtihani ya mwaka 2015, 2016 licha ya kuwepo kwa baadhi ya changamoto lakini matokeo yalikuwa mazuri na ya kupigiwa mfano.

Aliongeza kuwa hatua hiyo inatokana na kuwepo kwa elimu bure jambo ambalo limeasisiwa na Rais wa Mwanzo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume mara tu baada ya Mapinduzi ambapo pia, katika Ilani ya chama cha ASP elimu bure ilitiliwa mkazo.

Aidha, Dk. Shein aliwataka waalimu hao kufuata maadili ya kazi yao kwani kazi yao ni kazi iliyotukuka na wanaheshima kubwa katika jamii na kuwapongeza kwa kuchagua kazi hiyio ya uwalimu ambayo ni kazi yenye thawabu nyingi sana.

Pia, Dk. Shein alisisitiza haja kwa walimu kuwa na mbinu bora za kufundishia na kuwasaidia wanafunzi ikiwa ni pamoja na walimu kujiandaa kabla ya kufundisha na vile vile wawe tayari kujiendeleza kitaaluma na kujifunza kwa wengine wanaofanya vizuri.

Dk. Shein alisema kuwa kwa bahati mbaya katika baadhi ya skuli wapo walimu wachache wanaofanya kazi kwa kutegea kuwepo baadhi ya walimu wanaoingiza siasa katika kufundisha kwao jambo ambalo ni kinyume na wajibu na maadili ya uwalimu.

Pamoja na hayo, Dk. Shein  alisisitiza haja kwa waalimu wakuu kusimamia mazingira bora katika skuli kwa lengo la kupata matokeo mazuri sambamba na kusisitiza haja kwa walimu kuimarisha michezo katika skuli zao kwani Serikali imeanzisha Idara ya Michezo na Utamaduni kwenye Wizara ya Elimu kwa malengo maalum.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliwataka waalimu hao kupeleka salamu kwa jamii kuwa Srerikali imeamua kupambana na udhalilishaji wa wanawake na watoto na wale wote watakaokamatwa kwa kujihusisha na kosa hilo hakuna dhamana hadi kutakapotolewa hukumu.

Nae Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mmanga Mjengo Mjawiri alisisitiza haja kwa waalimu kuwa wabunifu, kuwana na amadili pamoja na heshima na kufuata muelekeo na mwennendo wan chi.

Mapema Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Khadija  Bakari Juma kwa niaba ya walimu na Wizara alitumia fursa hiyo kuungana na wananchi kumpongeza Dk. Shein kwa kutimiza mwaka mmoja wa uongozi wake katika kipindi cha Pili na kueleza mafanikio yaliopatikana katika sekta hiyo ya elimu ikiwa ni pamoja na ongezeko la skuli, madarasa, vitabu, vifaa vyenginevyo.

Katibu Mkuu huyo pia, alieleza kuwa Wizara hiyo ina kauli mbiu ya “Elimu Bora Kwanza” ikiwa ni msisitizo wa ubora wa elimu kwa wananfunzi wote na kueleza kuwa tayari Serikali imeshakamilisha ujenzi wa Skuli ya Msingi ya Mgonjoni, Skuli ya Sekondari ya Mohammed Juma Pindua ya Mkanyageni na Skuli ya Kwarara ambayo ina kituo cha kurushia matangazo ya redio na televisheni.

Aidha, alisema kuwa Serikali imeshatangaza zabuni za ujenzi wa skuli tisa za ghorofa zikiwemo skuli tano kwa upande wa Unguja na nne kwa upande wa Pemba  huku akieleza kuwa mchakato wa kumpata mkandarasi mwengine wa kuendeleza ujenzi wa Skuli ya Sekondari ya Kibuteni umekamilika na mkataba wa ujenzi unatarajiwa kusainiwa hivi karibuni.

Bi Khadija alieleza mafanikio zaidi yaliopatikana katika kiwango cha ufaulu katika mitihani ya taifa katika ngazi ya Kidato cha Pili, Kidato ca Nnne na Kidato cha Sita pamoja na ongezeko la wanafunzi waliopatiwa mikopo kupitia Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Zanzibar pamoja na mambo mengineyo katika sekta hiyo ya elimu.

Nao walimu hao walipata nafasi Ya kutoa risala zao kwa kila mkoa ndani ya mikoa yote miwili ya Pemba na kueleza mafanikio yaliopatikana katika sekta hiyo ya elimu pamoja na kueleza changamoto zilizopo.

Walimu hao pia, walipata fursa ya kutoa michago yao, maoni na ushauri kwa Dk. Shein kwa lengo la kuimarisha sekta elimu hapa nchini huku wakitoa pongezi zao kwa Rais Dk. Shein kwa kupata mshahara kwa wakati muwafaka.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk.
chanzo:zanzibar24.

Comments