Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali yakabidhi Vitabu vya Sheria mbalimbali kwa Idara ya Mahakama Zanzibar.

HABARIOfisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imekabidhi Vitabu vya Sheria mbalimbali ambazo zimeshafanyiwa Majumuisho ya Marekebisho mbalimbali kwa Idara ya Mahakama Zanzibar.
Vitabu hivyo vya Sheria vitaanza kutumika rasmi katika mahakama ikiwa ni mwendelezo wa kuzifanyia marekebisho sheria ambazo zimepitwa na wakati.

Mkuu wa kitengo cha uandishi wa Sheria Saleh Said Mubarak kwa niaba ya Mwanasheria mkuu amekabidhi vitabu hivyo kwa Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar Makungu ili vianze kutumika katika matumizi ya kila siku katika hafla iliyofanyika ukumbi wa Mahakama kuu Vuga mjini Zanzibar.


Mkuu huyo wa Kitengo cha uandishi wa Sheria amesema kuwa Sheria hizo zinahitaji umakini mkubwa kuweza kuzitumia hivyo ipo haja ya kutolewa mafunzo kwa watakaotumia sheria hizo kutokana na  utaratibu mpya uliowekwa katika sheria hizo.

‘’Si rahisi kuwa kila mwanasheria anaweza kuzielewa sheria hizo kwakuwa tu zimeandikwa katika vitabu, inahitaji umakini mkubwa kuweza kuzielewa’’. Alisema Saleh .

Aidha amefahamisha kuwa sheria zilizofanyiwa marekebisho zitaweza pia kupelekwa katika Ofisi za Muungano pamoja na tume za haki za binaadamu nchini.

Hata hivyo  amesema sheria hizo  zimefanyiwa marekebisho makubwa jambo ambalo limepelekea kuwa na vitabu vichache badala ya kuwa na vitabu vingi ambavyo vilikuwa vikitumika hapo awali.

Mwanasheria huyo amesema Sheria hizo hazikuvunja historia kilichofanyika ni  kuondolewa kwa zile sheria zisizofanya kazi na kuziacha zile zinazotumika kuweza kufanya kazi.

Sambamba na hayo ameleza kuwa Sheria hiyo imeweza kuandikwa kwa lugha nyepesi tofauti na mwanzo ili kuweza kuwawezesha wasomaji kuelewa kwa haraka .

Nae Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar Othman Makungu amesema Vitabu hivyo vitaisaidia sana Mahakama kuweza kufanya kazi zake kwa wepesi.

Amesema kuwa Vitabu hivyo pia vitaweza kuondoa changamoto kubwa kwa Mahakama na kwamba maboresho zaidi yatakuja kadiri mahitaji yatakapojitokeza.

Hata hivyo ameishukuru Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuweza kuwakabidhi vitabu hivyo ambavyo vitaweza kusaidia katika utekelezaji wa kazi zao.

chanzo: Zanzibar24.

Comments