‘Mshitakiwa kesi ya Malkia wa Pembe za Ndovu hakupigwa’.

Mahakama ya Hakimu Mkazi KisutuMKUU wa Kitengo cha Mashitaka katika Kituo cha Polisi Kijitonyama, Sajini Dismas Ngaraba (50) ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa alimkagua mshitakiwa Manase Philemon (39) kabla ya kumweka mahabusu na kwamba hakuwa na majeraha ya aina yoyote, bali alikuwa na afya nzuri.

Ngaraba alidai hayo mbele ya Hakimu Mkazi, Huruma Shaidi katika kesi ya meno ya tembo ya Sh bilioni 5.4 inayomkabili Philemon, raia wa China, Yang Feng Glan (66) maarufu kama ‘’Malkia wa Pembe za Ndovu’’ na mfanyabiashara Salvius Matembo.


Awali, Wakili wa Serikali Mkuu, Faraja Nchimbi alidai kuwa kesi hiyo imekuja kwa ajili ya kusikiliza kesi ndogo ndani ya kesi kubwa baada ya mshitakiwa Philemon kudai aliteswa na kupigwa wakati akichukuliwa maelezo.

Shahidi huyo alidai Aprili 20, 2014 kati ya saa 9 na saa 12 jioni alikuwa kituoni, na askari Beatus aliingia akiwa na mtu mmoja na kuingia katika Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi.

Alidai kuwa baadaye (Beatus) alimwambia amuweke mtuhumiwa mahabusu hadi upelelezi utakapokamilika, lakini mshitakiwa huyo alimwambia amuandikie maelezo kabla ya kuingia mahabusu.

Akiongozwa na Wakili Nchimbi, shahidi alidai kuwa saa 11:30 jioni, Beatus alimkabidhi mshitakiwa na kumueleza kuwa akae mahabusu kwa kujihusisha na biashara ya ujangili wa meno ya tembo.

Alidai kuwa kabla ya kumuingiza kwenye kitabu cha usajili namba 5 cha mwaka 2014, kwa ajili ya kumuweka mahabusu, Mkuu wa Upelelezi alimpa Ripoti ya Polisi (RB) na kumueleza kuwa Makao Makuu ya Polisi imeagiza mshitakiwa awekwe mahabusu kituoni hapo.

Aliendelea kudai kuwa alimsajili Philemon kwa namba 2033/2014 ambapo mshitakiwa alimwambia kuwa yeye ni mfanyabiashara na mkazi wa Ukonga.

Aliendelea kudai kuwa, utaratibu wao hawamuingizi mtuhumiwa mahabusu akiwa na matatizo ya kiafya na akikutwa nayo, anaenda kwa Mkuu wa Kituo au ofisa yeyote kwa ajili ya kupata maelekezo ikiwa ni pamoja na kupelekwa hospitali na endapo atalazwa atatakiwa kulindwa na kisha anatakiwa kurudi na vyeti kutoka hospitalini.

Aliieleza mahakama kuwa saa 12:40 mshitakiwa aliingia mahabusu na kwamba alikula na taarifa zake za afya alirekodi kuwa nzuri katika kitabu hicho.
chanzo:Habarileo.

Comments