Miradi ya umwagiliaji kufanyiwa mapitio.

Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Gerson Lwenge.SERIKALI inafanya mapitio wa miradi ya umwagiliaji yote nchini ili kubaini kwanini ilikwama kukamilika.

Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Gerson Lwenge alitoa kauli hiyo wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Mufindi Kaskazini, Mahmoud Mgimwa (CCM) aliyetaka kujua lini mradi wa umwagiliaji wa Ikweha, utaanza kufanya kazi.

Lwenge alisema miradi mingi ya umwagiliaji ilikwama kutokana na sababu mbalimbali zikiwamo zilizosababishwa na makandarasi.


“Miradi ya umwagiliaji maji, ilikwama kutokana na matatizo mbalimbali yakiwamo ya udhaifu wa usimamizi japo fedha zilitengwa kuendesha miradi hiyo,” alisema.

Alisema, pamoja na kufanya mapitio ya miradi hiyo, pia wizara yake inafanya usanifu wa miradi mipya ya umwagiliaji nchini ili kuanzisha miradi mingine mipya.

Akijibu swali la msingi la Mgimwa, Waziri Lwenge alisema mradi wa umwagijiliaji wa Ikweha, serikali ilitekeleza kwa awamu mbili, ya kwanza ilitumia sh milioni 435.9 na awamu ya pili ilitumia Sh milioni 370.7.

Lwenge alisema, baada ya kukamilika awamu hizo mbili kulikuwa na upungufu uliobainika na ulitakiwa kurekebishwa ndani ya kipindi cha matazamio cha miezi 12 kilichotarajiwa kukamilika Agosti mwaka jana.

“Kutokana na ucheleweshaji wa malipo kwa kazi alizozifanya mkandarasi huyo, iisababisha ucheleweshaji wa marekebisho ya upungufu huo,” alisema.

“Lakini Halmashauri ya wilaya ya mufindi na mkandarasi wamekubaliana marekebisho ya mradi huo yaanze kufanyika Aprili, mwaka huu,” alisema.
chanzo:Habarileo.

Comments