Mdee akwepa kutiwa pingu, aripoti Dodoma.

Mbunge wa Kawe, Halima MdeeMBUNGE wa Jimbo la Kawe, Halima Mdee (Chadema) ametii amri ya Spika wa Bunge, Job Ndugai aliyemtaka kuripoti kwenye Kamati ya Kudumu ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge.


Mdee na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani bungeni ambaye pia ni Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe walitakiwa na Spika kuripoti kwenye Kamati hiyo kwa kuwa walionesha vetendo vya utovu wa nidhamu.


Katika amri yake, Spika Ndugai alimtaka Mdee ambaye yupo nje ya mji wa Dodoma kuwa amewasili mjini hapa hadi kufikia saa 4.23 asubuhi leo ili kukutana na kamati hiyo vinginevyo Jeshi la Polisi limkamate popote pale alipo na afikishwe Dodoma akiwa amefungwa pingu.

Akizungumza baada ya kuwasili mjini Dodoma, Mdee alisema tayari ameshachukua samansi yake na yuko tayari kuripoti katika Kamati hiyo na kukabiliana na tuhuma zinazomkabili.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasilaino ya Bunge, Owen Mwandumbya, kamati hiyo ambayo ilikuwa ikutane nao jana, iliahirisha hadi leo kwa kile alichoeleza kwamba wabunge wanaounda kamati hiyo walikuwa katika shughuli nyingine za Bunge.

Spika alitangaza hayo bungeni juzi wakati akitoa majibu ya miongozo iliyoombwa na Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM) na Mbunge wa Madaba, Joseph Mhagama (CCM) ambao wote waliomba mwongozo kujua Spika anasemaje kuhusu vitendo vya utovu wa nidhamu uliofanywa na wabunge hao.

Mbowe na Mdee wanadaiwa kufanya vitendo hivyo wakati na baada ya kumalizika kwa uchaguzi wa wagombea wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) uliofanyika Aprili 4, mwaka huu.
chanzo:Habarileo.

Comments