Mbunge aomba msimamo kufungwa biashara.

Mbunge wa Tunduma, Frank Mwakajoka MBUNGE wa Tunduma, Frank Mwakajoka (Chadema) ameomba mwongozo kwa Naibu Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson katika kile alichosema Bunge litoe msimamo kwa kuwa wafanyabiashara wanafunga biashara kwa sababu ya ugumu wa mazingira.

Akijibu mwongozo huo, Dk Tulia amesema Bunge haliwezi kutoa msimamo wa suala hilo kwa vile pamoja na kuwa zipo biashara zinazofungwa kwa ugumu wa mazingira ya kufanya biashara, lakini zipo pia zinazoanzishwa.


Awali akiomba mwongozo huo, Mwakajoka alisema; “Mheshimiwa Naibu Spika zipo taarifa kwamba wafanyabiashara wanafunga maduka yao, mahoteli yao.

“Hatua hii mheshimiwa Naibu Spika inasababisha serikali ipoteze mapato mengi ambayo yangetokana na kodi kama biashara hizi zingeendelea kuwepo na hadi sasa hakuna utatuzi wowote wa jambo hili. Nataka tu kufahamu katika hili, Bunge linaweza kuchukua hatua gani ili kuweza kuisimamia serikali iweze kurekebisha hali hiyo?”

Naibu Spika akijibu alisema pamoja na kuwa mbunge huyo ameomba mwongozo huo kinyume cha utaratibu kutokana na Kanuni kusema wabunge wataomba mwongozo kutokana na jambo lililotokea mapema bungeni, lakini suala hilo limewahi kutolewa majibu bungeni.

"Waheshimiwa wabunge suala hili halipo kabisa katika shughuli za leo hata katika maswali yaliyoulizwa leo hakuna mahali suala hili limejitokeza. Kwa hiyo si la mapema leo.

"Lakini niseme wazi kama ambavyo Naibu Waziri wa Fedha na Mipango amewahi kusema hapa bungeni siku zilizopita, wakati zipo biashara zinafungwa lakini zipo zinazofunguliwa pia," alisema Naibu Spika.

Katika hatua nyingine, Mbunge wa Buyungu, Samson Bilago (Chadema) aliomba mwongozo kwa Spika akitaka kufahamu ni kwa nini Bunge halikumchukulia hatua Mbunge wa Ulanga, Goodluck Mlinga aliyetumia lugha ya kuudhi wakati akichangia bungeni.

Akitumia Kanuni ya 64 (1) vipengele vidogo vya (f) na (g), Mbunge huyo alisema Mlinga akichangia bungeni alisema alishindwa kufahamu ni nani alikuwa mgombea mwanamke kwa kiti cha Bunge la Afrika Mashariki (EALA) kutoka Chadema kati ya Lawrence Masha na Ezekia Wenje.

Bilago alisema hatua ya mbunge huyo kutoa matamshi hayo ya kuudhi bila Bunge kumchukulia hatua ilikuwa ni sawa na kuwalinda wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) huku wabunge wa upinzani wakishughulikiwa.

Hata hivyo, Naibu Spika alisema asingeweza kutolea mwongozo suala hilo kwa vile si jambo la mapema na kuwa hata siku Mlinga alipotoa maneno hayo hakuwepo katika kiti cha Spika.
chanzo:Habarileo.

Comments