Manyara yaongoza ukeketaji kwa 100%.

UTAFITI uliofanywa na Serikali umebaini kuwa ukeketaji upo kwa asilimia 100 katika maeneo ya vijijini mkoani Manyara. Hayo yalisemwa bungeni jana na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Hamisi Kigwangalla alipokuwa anajibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Martha Umbula (CCM).

Umbula alitaka kujua wilaya na vijiji vinavyoongoza kwa mila potofu ya ukeketaji wanawake kama ulivyooneshwa katika takwimu za utafiti uliofanywa mwaka 2010 na kubaini mkoa wa Manyara ndio kinara wa ukeketaji nchini. Alitaja pia kujua athari na idadi ya vifo mkoani Manyara, lakini pia mkakati wa dharura wa kukabiliana na mila hiyo potofu ili kuondoa kabisa athari za ukeketaji.


Akijibu, Kigwangalla alisema katika utafiti huo, ni kweli Manyara ilibainika kuwa na ukeketaji kwa asilimia 100 hasa maeneo ya vijijini na kuongeza kuwa, wilaya zote za mkoa wa Manyara zinajihusisha na vitendo hivyo, hasa wilaya ya Hanang. Aliyataja makabila yanayofanya ukeketaji katika wilaya hiyo kuwa ni Wairaki, Wabarbaig na Wanyaturu, wengi wakiwa katika maeneo ya Kata za Balanglalu na Basutu.

Akizungumzia athari, alisema ni kubwa sana kwa wanawake hasa wakati wa kujifungua, kwani huweza kusababisha ulemavu wa kudumu, vifo kutokana na kutokwa na damu nyingi, maumivu makali, kupatwa ugonjwa wa fistula na wakati mwingine kupata madhara ya kisaikolojia. Alisema ni vigumu kutambua vifo vinavyotokana na ukeketaji, kwani hufanyika kwa siri katika jamii hiyo. Kuhusu kukabiliana na tatizo hilo, alisema Serikali imetunga sheria mbalimbali.

Hata hivyo, alisema sheria pekee bila elimu kwa umma haiwezi kumaliza tatizo hilo. 

Aliongeza kuwa, kwa sasa wanatumia zaidi maofisa maendeleo wa ustawi wa jamii ili kuhamasisha na kutoa elimu kwa wananchi kuondokana na mila na tamaduni hizo. Aliwataka pia wabunge na viongozi mbalimbali kushiriki katika kuhamasisha wananchi kuondokana na mila hizo.
chanzo:Habarileo.

Comments