Maghembe apiga marufuku usafirishaji mkaa.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe akifungua mkutano wa 24 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara yake uliofanyika katika ukumbi wa LAPF mjini Dodoma. Kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk Aloyce Nzuki na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Esther Malima. (Picha na Hamza Temba, Wizara ya Maliasili na Utalii).WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe ametangaza mabadiliko muhimu katika biashara ya mkaa nchini na kubainisha kuwa agizo la kutosafirisha mkaa kutoka wilaya moja kwenda nyingine ili kunusuru misitu inayoteketea kwa kasi nchini litaanza kutekelezwa rasmi Julai.

Aidha, amepiga marufuku kuanzia leo usafirishaji wa mazao ya misitu ndani na nje ya nchi kwa kutumia nakala zisizo halisi, kuunga mkono Sera ya Uchumi wa viwanda ya Serikali ya Awamu ya Tano hakuna gogo litakalosafirishwa kwenda nje ya nchi.


Amesema hayo wakati akifungua Mkutano wa 24 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Maliasili na Utalii, uliofanyika kwenye Ukumbi wa LAPF mjini Dodoma na kuhudhuriwa na wajumbe mbalimbali kutoka kwenye Idara, Vitengo na Taasisi mbalimbali zilizopo chini ya wizara hiyo.

“Kuanzia mwezi Julai hakuna ruhusa ya kutoa vibali vya kuhamisha mkaa kutoka wilaya moja kwenda wilaya nyingine, mkaa utachomwa, utauzwa ndani ya wilaya kwa ajili ya matumizi ya Watanzania wanaohitaji nishati ya mkaa, lakini biashara ya mkaa ya kutoa Dodoma kwenda Dar es Salaam mpaka Zanzibar marufuku.

“Wamekata misitu yetu yote, mito yetu imekauka, tunashindwa kupata maji ya umwagiliaji kwa sababu watu wengi huko nje wanataka mkaa wetu, Tanzania jamani sio shamba la bibi, wale wote watakaotoa mkaa kutoka eneo moja hadi jingine kinyume na sheria hii watashuulikiwa kwa utaratibu wa uhujumu uchumi,” alisema Maghembe.

Alisema kwa upande wa miji mikubwa kama Dar es Salaam, Dodoma, Morogoro na Tanga vitaanzishwa viwanda maalumu vya kuzalisha mkaa ambao utauzwa kwa vibali maalumu katika mikoa mbalimbali nchini.

Alisema mkaa huo hautakuwa na athari nyingi za kimazingira kwa sababu utazingatia taratibu za uzalishaji endelevu.

Aidha, amemuagiza Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kumhamisha kituo cha kazi Mkuu wa Kikosi cha Kufuatilia na Kuzuia Uharibifu wa Misitu, Arjason Mloge kutoka Makao Makuu ya TFS kwenda Chuo cha Viwanda vya Misitu (FITI) mkoani Kilimanjaro na badala yake atafutwe mtu mwingine muaminifu.

Alisema uamuzi huo ni kufuatia udhaifu uliojitokeza katika usafirishaji wa rasilimali za misitu ndani na nje ya nchi ikiwemo usafirishaji kwa kutumia nakala za vibali ambazo sio halisi, yaani za kudurufu.

“Agizo hili litekelezwe mara moja kabla ya saa sita mchana wa leo (jana) na niwe nimepewa nakala ya barua hiyo ya uhamisho,” alieleza.

Kutokana na uamuzi huo, amepiga marufuku kuanzia leo usafirishaji wa mazao ya misitu ndani na nje ya nchi kwa kutumia nakala zisizo halisi.

Ameongeza kuwa katika kuunga mkono Sera ya Uchumi wa Viwanda ya Serikali ya Awamu ya Tano, hakuna gogo litakalosafirishwa kwenda nje ya nchi.

“Wawekezaji wanahimizwa kujenga viwanda vya kuchakata magogo hayo hapa nchini ili kutoa ajira kwa Watanzania pamoja na kutoa faida halisi inayotokana na rasilimali hizo kwenye uchumi wa taifa,” alieleza waziri huyo.

Akizungumzia changamoto ya mifugo kwenye maeneo ya hifadhi nchini, alisema Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori Namba 5 ya mwaka 2009 sehemu ya 21 (1) hairuhusiwi kabisha kuchunga mifugo katika Hifadhi za Taifa, Mapori ya Akiba, Mapori Tengefu na Hifadhi za Misitu.

Amewataka watumishi wa Maliasili kusimamia sheria hiyo pamoja na kutoa mwito kwa wananchi kuifuata kikamilifu.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Dk Aloyce Nzuki alimueleza Waziri Maghembe kuwa maelekezo yote aliyoyatoa yamepokelewa kwa ajili ya kuyafanyiwa kazi, huku Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Profesa Alexander Songorwa akimueleza waziri huyo kuwa watalinda na kusimamia Maliasili za Taifa na kwamba katu hawapo tayari kuandikwa kwenye vitabu kuwa walishiriki katika kutoweka kwa maliasili hizo.
chanzo:Habarileo.

Comments