Kenyatta awaonya wanaofanya njama za kuvuruga uchaguzi Kenya.

Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya amewaonya watu aliosema wanafanya njama za kuvuruga Uchaguzi Mkuu wa mwezi Agosti mwaka huu.

Rais Kenyatta amewaambia waandishi wa habari kwamba, hatovumilia kitendo chochote cha kuchochea machafuko na kwamba sheria itamuadhibu vikali mtu yeyote atakayochochea machafuko na kujaribu kuvuruga uchaguzi huo.

Uchaguzi Mkuu unatarajiwa kufanyika tarehe 8 Agosti mwaka huu nchini Kenya. Ikumbukwe kuwa nchi hiyo ilishuhudia machafuko mabaya ya umwagaji wa damu baada ya uchaguzi mkuu wa tarehe 27 Disemba 2007. Mamia ya watu waliuawa na wengine wengine kupoteza makazi yao katika machafuko hayo.
Hivi sasa pia hali ya uchaguzi nchini Kenya ni ya wasiwasi kiasi kwamba machafuko yamekuwa yakiripotiwa katika chaguzi za michujo ya wagombea za vyama vya kisiasa nchini humo.
Aidha, hadi hivi sasa muungano wa upinzani wa NASA umeshindwa kutangaza mgombea wao kutokana na kila chama kutaka mkuu wake ateuliwe kugombea urais, suala ambalo linazidisha homa ya uchaguzi nchini humo. Karibu Wakenya milioni 19 wametimiza masharti ya kupiga kura.
chanzo:parstoday.

Comments