Hata hivyo, imeelezwa kuwa, kuchelewa kwa hatua hiyo kumetokana na
dhamira njema ya Serikali ya Awamu ya Tano kutaka kuboresha mifumo na
miundo ya kiutendaji nchini.
Akihutubia Bunge baada ya kuapishwa Novemba 5, 2015, Rais John
Magufuli alisema Serikali yake inatambua mchakato wa kupata Katiba mpya
na itaendelea nao.
Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi, ameiambia
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuwa, Serikali ya Awamu ya
Tano inatambua umuhimu wa nchi kuwa Katiba mpya.
“Hata hivyo ikumbukwe kuwa mara baada ya Serikali ya Awamu ya Tano
kuingia madarakani, ilianza kazi kwa kuunda serikali, uhakiki wa
watumishi hewa, uadilifu na kupunguza Baraza la Mawaziri ili kuongeza
uwajibikaji,” alisema Profesa Kabudi.
Alisema ingawa lengo la serikali halikuwa kupunguza idadi tu ya
watendaji na viongozi, lakini kupunguza idadi ya mawaziri kutoka 60 hadi
18 ni moja ya dhamira ya mageuzi katika utendaji na uwajibikaji.
Alisema hivi sasa, baada ya kazi hiyo kukamilika, Serikali inapitia
sheria zote zinazohusika na mchakato huo wa mabadiliko ya Katiba kubaini
utaratibu mzuri wa kuendelea na mchakato huo kutoka pale ulipoishia,”
alisema.
Profesa Kabudi alieleza hayo wakati akijibu hoja za wajumbe wa Kamati
hiyo ya Bunge ya Sheria na Katiba kuhusu mchakato huo baada ya
kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa bajeti ya wizara yake kwa mwaka wa
fedha 2016/17 na mapendekezo kwa mwaka 2017/18 mbele ya kamati hiyo
mjini hapa.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kuwasilisha taarifa hiyo,
Profesa Kabudi alisema: “Serikali inalipa uzito mkubwa suala la Katiba
mpya, ila serikali ilikuwa na kazi ya kuunda mifumo na baadhi ya mageuzi
ya kimfumo yamegusa matakwa ya Bunge Maalum la Katiba kuhusu Katiba
mpya ambalo nami nilikuwa mjumbe.
“Hivi sasa kutokana na mabadiliko ya sheria mbalimbali, maboresho ya
uadilifu serikalini ambao wajumbe wa Bunge la Katiba mpya walilipigia
kelele sana tayari limetekelezwa na aina namna ya utendaji makosa sasa
imebadilika si kama miaka 20 iliyopita.
“Aina ya uchumi nayo imebadilika kutoka katika mfumo wa ujamaa na
chama kimoja hadi wakati tulio nao sasa, matamanio ya rushwa
yameongezeka na kazi ya kuyadhibiti inaonekana, wakati haya yakiendelea
kufanywa na Serikali, suala zima la kupitia na kushauri Serikali namna
njema ya kuendelea na mchakato, linaendelea,” alisema Profesa kabudi.
Alifafanua kuwa, lengo kubwa la Katiba ni kuleta mabadiliko katika
sekta zote nchini, na baadhi yameanza kuonekana ikiwemo maadili ya
viongozi wa umma yamerejea na sasa viongozi wanatamka viapo na
kuvisaini.
Wakati wa wajumbe wa kamati wakijadili, Mbunge wa Bahi, Omary Badwel
(CCM) alishangaa kwa nini wizara haijatenga muda maalum wa kukamilisha
kupatikana kwa Katiba mpya wakati ipo wazi katika Ilani ya CCM ya
2015-2020.
“Jamii ina matarajio makubwa ya kupatikana kwa Katiba mpya kabla ya
awamu hii ya uongozi kwa kuwa Ilani ya CCM imeahidi hayo lakini Serikali
imekaa kimya kuhusu muda, haijaainishwa wazi lini tutapata hiyo Katiba
mpya katika mpango wa wizara. “Tunahitaji kuona mchakato wa kupata
Katiba mpya unakamilika ndani ya awamu hii,” alisema Badwel.
Akijibu hoja hiyo ya Badwel, Profesa Kabudi alisema kama
alivyofafanua katika taarifa, mchakato utaendelea lakini yeye kwa kuwa
ni mgeni kwenye wizara, hawezi kueleza ni lini.
“Nadhani kwa kuwa mimi ni mgeni katika wizara, nitayachukua haya
maana hata Waziri Mkuu zijamuona, vikao vya Baraza la Mawaziri sijakaa.
Makamu wa Rais nimeonana naye siku ya kuapishwa. Naomba niahidi
kulifanyia kazi zaidi hili,” alisema Profesa Kabudi.
Katiba mpya itakapokamilika, itaiondoa Katiba ya mwaka 1977
inayotumika hivi sasa ambayo wakati ikitungwa, mfumo wa uongozi nchini
ulikuwa ni wa chama kimoja.
Hata hivyo Katiba hiyo imefanyiwa marekebisho kadhaa kukidhi kwa sehemu kubwa mahitaji ya wakati huu.
Miongoni mwa wadau wanaosimamia kupata Katiba mpya ni Jukwaa la
Katiba Mpya, ambalo limeendelea kuishauri Serikali kutenga fedha maalum
katika kipindi cha mwaka wa fedha 2017/18 kwa ajili ya kuendelea na
mchakato wa kupata Katiba mpya, hatua ya kura za maoni kwa Watanzania.
Waziri Kabudi aliwasilisha taarifa kwa kamati inayoonesha kuwa wizara
hiyo inahitaji bajeti ya Sh bilioni 159.31 ikiwa na upungufu wa
asilimia 4 ya bajeti ya mwaka jana ya Sh bilioni 191.4.
chanzo:Habarileo.
Comments