Jukwaa la Biashara Mkoa wa Mwanza: Zaidi ya watu 300 kubadilika kimtazamo.

Mandhari ya jiji la Mwanza linavyoonekana kutokea katika mzunguko wa Uhuri jijini humo. Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) wachapishaji wa magazeti ya Daily News, Habarileo na Spotileo limeandaa Jukwaa la Biashara jijini Mwanza litakalo fanyika Aprili 11 mwaka huu kwa kushirikana na ofisi ya Mkuu wa Mkoa lengo likiwa ni kuainisha fursha za uwekezaji mkoani humo. (Picha na Mroki Mroki).JUMANNE ya Aprili 11, watu wanaokadiriwa kuwa zaidi ya 300 wataketi kwenye viti vyao katika ukumbi mkubwa na wa kisasa wa Rockcity Shopping and More wa jijini Mwanza, kusikiliza mada motomoto zitakazowasilishwa na wadau mbalimbali wa maendeleo.

Hili ni Jukwaa la pili la Biashara lililoandaliwa na Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) kwa kushirikiana na ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza. Jukwaa la kwanza kuandaliwa na TSN lilifanyika Februari 13 mkoani Simiyu na kuhudhuriwa na watu takribani watu 160.


Makundi mbalimbali kuhudhuria Maandalizi kamambe yanayoendelea hapa mkoani Mwanza yanaonesha kwamba washiriki wanaotazamiwa kuketi kwa saa kadhaa wakifaidikia na uwepo wa Jukwaa hilo la Biashara ni pamoja na wafanyabiashara wadogo wakiwemo madereva wa bodaboda, teksi na daladala.

Pia kutakuwa na wauza bidhaa kwenye masoko mbalimbali mkoani Mwanza, wauza mitumba na wauza samaki na dagaa. Kwa mujibu wa Mhandisi Boniface Nyambele anayeratibu Jukwaa hilo kwa upande wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Patrice Simbachawane wa TSN, wengine walioalikwa ni wafanyabiashara wakubwa na wa kati, wafanyabiashara wanawake na wamiliki wa viwanda.

Mkoa wa Mwanza una viwanda 86 kwa mujibu wa Kitengo cha Uwekezaji mkoani Mwanza kinachoongozwa na Mhandisi Nyambele sambamba na maofisa wengine waandamizi sita.

Waratibu hao tayari wamesambaza pia barua za mwaliko kwa wawakilishi wa taasisi mbalimbali za elimu mkoani Mwanza, maofisa mbalimbali wa taasisi za serikali, maofisa wa halmashauri nane za mkoa wa Mwanza, wakuu wa wilaya, wabunge na wakuu wa mikoa ya jirani.

Wengi watajaribu uwekezaji mkubwa Akizungumzia matarajio yake kuhusua Jukwaa hilo, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella anasema ana matumaini makubwa kwamba litawazindua wafanyabiashara wazawa kufikiria kufanya makubwa zaidi kwa faida yao, mkoa na taifa kwa ujumla.

Anasema anatamani kuona wafanyabiashara wadogo wanatumia fursa zilizopo kwa kuwekeza pakubwa na hivyo kuwa pia wafanyabiashara wakubwa.

Mkuu huyo wa mkoa anasema pamoja na kukaribisha wawakezaji wengine kutoka nje ya mkoa na hata nje ya nchi, angetamani kuona wawekezaji wa mkoani mwake wanakuwa wa kwanza kunufaika na fursa zilizopo.

“Kimsingi, tunao wawekezaji wengi wazalendo na wazawa wa hapa Mwanza. Na hata pesa wanazo lakini bado wanahangaika na vitu ambavyo havina tija kubwa kwao wenyewe, kwa mkoa na taifa kwa ujumla.

Tunataka jukwaa hili lisaidie kuwabadilisha, wazione fursa na kuwa wawekezaji wakubwa. “Kwa lugha nyingine, wawekezaji wa ndani (hapa mkoani Mwanza) wapo lakini tatizo lao ni namna gani waingie kwenye uwekezaji mkubwa. Nina imani kwamba jukwaa litasaidia kuwabadilisha hawa wawekezaji wetu wa ndani,” anasema.

Mkuu huyo wa mkoa anawakaribisha wote waliopata mwaliko na watakaoendelea kupata wahakikishe hawakosi kuhudhuria jukwaa hilo adhimu kwa ajili ya maendeleo yao na ya mkoa kwa ujumla. Baadhi ya wadau watakaotoa elimu muhimu kwa wafanyabiashara ni pamoja na benki za NMB, TIB (Development), TIB (Corporate) na Benki ya TPB.

Taasisi hizi za fedha zinatazamiwa kueleza, pamoja na mambo mengine, namna wafanyabiashara wanavyoweza kupata fedha za mitaji alimradi waweze kutekeleza masharti fulani fulani.

Ni uelewa kwa kwenda mbele Katika Jukwaa la Simiyu, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TIB (Corporate), Frank Nyabundege alisema kwamba mtu akitekeleza masharti ya benki hiyo ambayo pia inatoa huduma ya kuandaa maandiko ya miradi kitaalamu, anaweza kupata mkopo ndani ya siku mbili.

Nyabundege akaweka wazi kwamba benki yao ndio ipo mahususi kwa ajili ya suala zima la kutekeleza dhana ya viwanda inayotekelezwa na serikali ya awamu ya tano.

Naye Kaimu Mkuu wa Kitengo cha wateja wakubwa wa NMB, Nsolo Mlozi, atakuwepo Mwanza kuongeza uelewa kwa Watanzania hao zaidi ya 300 kuhusu masuala mbalimbali ya kibenki na namna wanavyoweza kupata mitaji kupitia NMB.

Hivi karibuni alipozungumza na HabariLeo, Mlozi alisema: “Cha muhimu ni uelewa kwa wananchi... 
Tunakwenda pia kulifanya hilo (la kuamsha uelewa) Mwanza.” Mamlaka ya Mapato (TRA) ni mdau mwingine wa maendeleo anayetazamiwa kutoa elimu muhimu kwa mlipa kodi.

Kama ilivyotokea Simiyu, ni taasisi inayotazamiwa kuulizwa maswali mengi na wafanyabiashara Taasi hiyo inaamini kwamba wananchi wengi wanao utayari wa kulipa kodi kwa ajili ya maendeleo ya nchi yao alimradi tu wajue taratibu muhimu na kanuni.

Wakati Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) linatazamiwa kueleza mengi namna wana- Mwanza wanavyoweza kulitumia katika kufanikiwa, Bohari ya Dawa (MSD) itaeleza, pamoja na mambo mengine, namna ambavyo watu binafsi wanaweza kununua vifaa tiba kutoka kwenye bohari hilo badala ya kuhangaika kwenye maduka binafsi.

Bila afya, huwa ngumu kuendesha biashara kwa ufanisi hivyo Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), utatumia jukwaa hilo kueleza namna wafanyabiashara na makundi mbalimbali ya wajasiriamali wanavyoweza kufaidika nao, wakapata matibabu hata wakati ambao hawana fedha mfukoni.

Katika muktadha huo wa afya, taasisi ya Ariel Glaser Pediatric Aids Healthcare Initiative (AGPAHI), pamoja na mambo mengine, itawajuza washiriki kwamba ili nguvu kazi iwe na manufaa ni lazima iwe na afya njema.

Miongoni mwa mengi yatakayosemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa AGPAHI, Dk Sekela Mwakyusa ni: “Tumekuwa huku Kanda ya Ziwa kwa muda sasa, tumejionea mengi mintarafu suala zima la Ukimwi lilivyo. Wengi hawajui hali ilivyo.”

Watumishi Housing Company (WHC) itaeleza namna inavyojenga nyumba za kisasa katika eneo la Kisesa mkoani Mwanza na jinsi inavyopania kuwawezesha watu binafsi kununua hisa (vipande) katika kuchangia makazi bora.

Nao Mfuko wa Pensheni wa LAPF utawataka wawekezaji wachangamkie kukodi maduka katika ukumbi wa Rockcity Shopping and More kwani bado yapo yaliyo wazi ili kupata mafanikio makubwa kibiashara. Pia wataeleza mafao wanayotoa kwa wafanyakazi wanaojiunga na mfuko huo.

Baraza la Biashara Tanzania litakuwa na mengi ya kuzungumza na wafanyabiashara wenzao huku Kampuni ya Simu (TTCL) ikielezea jinsi wafanyabiashara wanavyoweza kufaidika nayo kupitia bidhaa nyingi inazotoa kwa sasa.

Je, ni wangapi wanajua kwamba TTCL imeanzisha huduma ya kutuma pesa na ambayo ina faida maradufu kwa mteja? Je, unajua kwamba ukitaka kujiunga na mkonga wa taifa ni suala la kuwasiliana nao tu bila kuuhangaika kwingineko?.

Kampuni ya simu ya Vodacom, moja ya mitandao pendwa nchini pia itaeleza namna inavyorahisisha maisha hususani kwa wafanyabiashara huku Mfuko wa Pensheni wa PPF ukieleza mafao mengi ambayo watanzania wanaojiunga nao wanafaidika. Mengi zaidi kuhusu Jukwaa la Biashara Mwanza endelea kusoma HabariLeo.
chanzo:Habarileo.

Comments