Gwajima na wenzake kujitetea kortini leo.

KESI ya kushindwa kuhifadhi silaha inayomkabili Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima na wenzake itaendelea kunguruma leo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, ambapo washitakiwa hao watajitetea.

Wakili wa Serikali, Joseph Maugo alidai jana mbele ya Hakimu Mkazi, Godfrey Mwambapa kuwa kesi hiyo imekuja kwa ajili ya kusikiliza na kwamba upande wa mashitaka upo tayari kuendelea.


Hata hivyo, Hakimu Mwambapa alisema hakimu anayesikiliza kesi hiyo, Thomas Simba hayupo hivyo itaendelea kusikilizwa leo.

Mbali na Gwajima, washitakiwa wengine ni Askofu Msaidizi wa kabisa hilo, Yekonia Bihagaze, mfanyabiashara George Mzava na mkazi wa Kimara Baruti, Geoffrey Milulu.

Washitakiwa hao wanadaiwa walikutwa na begi likiwa na vitu mbalimbali ikiwamo risasi 17 na bastola. Awali, katika utetezi wake, Gwajima alidai kuwa Machi 27, 2015 alikuwa safarini kuelekea Arusha kwenye kikao cha maaskofu, na aliondoka Dar es Salaam, Machi 26, 2015.

Alidai kuwa wakati alipokuwa njiani kuelekea Arusha aliona taarifa kwenye mtandao wa kijamii kuwa Askofu Gwajima anatafutwa na Jeshi la Polisi.

Alieleza kuwa alishangaa kuiona taarifa hivyo, hivyo akafika hadi Arusha, lakini alishindwa kushiriki katika mkutano huo badala yake alianza safari ya kurudi jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kwenda kwenye Kituo Kikuu cha Polisi Kanda ya Dar es Salaam kwa ajili ya kuripoti na ndipo kesi hiyo ikafunguliwa na kuendelea kusikilizwa na watuhumiwa kutakiwa kujitetea leo.
chanzo: zanzibar24.

Comments