Katika mwaka wa fedha 2016/2017, Wizara hiyo iliidhinishiwa na Bunge
bajeti ya Sh bilioni 191.45 na sasa wizara inaomba iidhinishiwe Sh
bilioni 159.33 ikiwa na upungufu huo.
Wakati bajeti hiyo ikionesha upungufu huo, baadhi ya wajumbe wa
kamati hiyo wamehoji kwanini wizara inaomba bajeti pungufu wakati katika
baadhi ya ofisi za taasisi zilizo chini yake, ikiwemo ya Tume ya Haki
za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) visiwani Zanzibar, Pemba,
inapelekewa fedha za matumizi mengineyo (OC) ya Sh 100,000 tu kwa mwezi.
Akiwasilisha taarifa hiyo mbele ya Kamati hiyo, Waziri wa Katiba na
Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi, alisema katika bajeti ya mwaka jana
hadi kufikia Desemba 2016, walikuwa wamepokea Sh bilioni 97.2 sawa na
asilimia 51 ya bajeti nzima.
Profesa Kabudi alisema mwaka huu wa fedha kumekuwa na upungufu kwa
kuwa bado katika fedha zinazotolewa na wahisani na washirika wa
maendeleo, hazijajumlishwa katika bajeti kwa kuwa bado mazungumzo
yanaendelea.
“Mtakumbuka juzi hapa tulikuwa na ugeni wa Rais wa Benki ya Dunia na
Rais wetu, John Magufuli alieleza hilo, sasa haya ni baadhi ya
mazungumzo yanayoendelea na matumaini ni makubwa,” alisema Profesa
Kabudi.
Alisema sababu nyingine ya kupungua kwa bajeti hiyo ni ukomo wa
bajeti kupungua kwa asilimia 55 lakini ongezeko limekuwepo kwa asilimia
11 katika fedha za mishahara na Fedha za OC kwa asilimia 26 mwaka
2017/2018.
Baadhi ya wajumbe wa Kamati hiyo akiwemo Mbunge wa Malindi, Ali Saleh
Ali (CUF) na Mbunge wa Viti Maalum, Riziki Lulida (CUF) walihoji kwa
nini ofisi ya THBUB haiboreshewi fedha za OC na kuifanya kushindwa
kutekeleza majukumu yake ipasavyo.
Saleh alisema walipotembelea visiwani Pemba hivi karibuni, walikuta
fedha ya OC katika ofisi hiyo kwa mwezi ni Sh 100,000 huku kukiwa na
mtumishi mmoja katika ofisi ambaye anafanya kazi zote kazi za Tume,
usimamizi na usafi wa ofisi.
“Hatumtendei haki kiongozi wa hii tume, haiwezekani tume inayosimamia
masuala ya haki za watu nchini na ndio mwakilishi wetu kimataifa wa
haki hizo haboreshewi OC, hii si sawa kabisa,” alisema Lulida.
chanzo:Habarileo.
Comments