Zanzibar yatakiwa kuchangamkia fursa za ushirikiano na India.

Zanzibar imeshauriwa kuchangamkia fursa mbalimbali za ushirikiano zinapotokezea baina yake na Serikali za Majimbo Nchini India zikiwemo sekta za Kilimo, Biashara, Uwekezaji, Afya na huduma za Mawasiliano kutokana na Taifa hilo liliopo Barani Asia kupiga hatua kubwa ya Maendeleo kwenye Sekta hizo.

Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Balozi wa Tanzania Nchini India Balozi Mohamed Hija wakati akikiongoza Kikao cha matayarisho cha  Ujumbe wa Zanzibar
unaoongozwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ambao tayari umeshawasili Nchini humo kwa Ziara ya Kiserikali ya Wiki Moja.

Balozi Mohamed Hija alisema Zanzibar ina fursa pana  ambazo bado haijazitumia katika kujitanua kimawasiliano kwa kushirikiana na Taasisi  mbalimbali Duniani katika harakati zake za kujikwamua kiuchumi na kuimarisha mipango yake ya Maendeleo hasa kwenye zile Sekta zilizo nje ya Muungano.

Alisema India imebarikiwa kuwa na Taasisi na Makampuni mengi kwenye Serikali za Majimbo ambazo zinaweza kusaidia nguvu za Kiuchumi Visiwani Zanzibar iwapo mipango ya uhakika itawekwa ukiwemo utaratibu maalum wa kufuatilia makubaliano yanayofikiwa ya pande mbili husika.

Balozi Hija aliueleza Ujumbe huo wa Zanzibar kwamba Ofisi ya Ubalozi Nchini India iko tayari kuratibu masuala yote yatayohusika na mikataba au makubaliano baina na Zanzibar na Taasisi au Serikali ya Jimbo lolote Nchini humokatika  uanzishwaji wa ushirikiano wa kisekta.

Alifahamisha kwamba ipo miradi inayofikia hatua ya kutiwa saini katika uanzishwaji wake lakini kinachokosekana kuibuka kwa miradi hiyo na hatimae mengine kufifia ni ukosefu wa ufuatiliaji wa miradi hiyo jambo ambalo huwavunja moyo wale wanao nia thabiti ya kusaidia.

Balozi Hija alielezea faraja yake kutokana na ujio wa Ujumbe huo wa Zanzibar Nchini India na kusema kwamba huo  ni mwanzo mzuri wa kufungua njia itakayotoa mwanga kwa Zanzibar kujitanua zaidi kiuchumi Kimataifa.

Naye kwa upande wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema ziara hiyo ina lengo la kutengeneza Diplomasia juu ya ushirikiano kati ya Zanzibar na India hasa katika sekta za Afya, Kilimo, Biashara na hata Utalii.

Balozi Seif alisema India imekuwa mshirika mkubwa wa Zanzibar katika Sekta ya Afya kiasi kwamba wagonjwa wengi wa Zanzibar wanaosumbuliwa na maradhi tofauti kama  Moyo, Figo pamoja na magonjwa mengine hupata
huduma za matibabu katika Hospitali za India.

Othman Khamis Ame.
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
19/3/2017.
chanzo: zanzibar24.

Comments