Waziri: Utafutaji mafuta hautaathiri mazingira.

Waziri wa Maji, Nishati, Ardhi na Mazingira, Salama Aboud TalibSERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imewatoa hofu wananchi na kusisitiza itahakikisha mazingira ya wananchi pamoja na maslahi yao katika kazi za utafutaji wa mafuta na gesi ambazo zimeanza sasa, yanalindwa.

Waziri wa Maji, Nishati, Ardhi na Mazingira, Salama Aboud Talib alisema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari baada ya kuanza kwa kazi za utafiti wa nishati ya mafuta na gesi kwa kutumia ndege, itakayoruka hewani na kupiga picha mbali mbali katika maeneo ya ardhi.


Alisema suala la mazingira limepewa kipaumbele cha kwanza katika kazi za mafuta, na sehemu ambayo nishati hiyo itagundulika, maslahi ya wananchi yatazingatiwa kwa kiwango kikubwa.

Alifafanua kuwa, maslahi yao yatalindwa ikiwemo kulipwa fidia baada ya kuhamishwa na kupisha kazi za uchimbaji wa mafuta na gesi.

“Kazi za utafutaji wa mafuta na gesi zimeanza rasmi na tunawahakikishia wananchi kwamba maslahi yao yatalindwa kwa sababu tutazingatia uhifadhi wa mazingira katika zoezi hilo,” alisema.

Alisema makubaliano na kampuni itakayofanya kazi za utafiti yamezingatia maslahi mapana ya wananchi, hivyo hakuna matatizo yanayoweza kujitokeza wakati kazi za utafutaji mafuta zikifanyika nchini.

Aidha, alisema Serikali bado inaendelea na utafiti wa kazi ya utafutaji nishati mbadala ikiwemo umeme wa jua na mawimbi ya bahari ili kuifanya Zanzibar kuwa na nishati ya uhakika.

Alisema tafiti hizo zinaendelea kufanywa kwa kushirikiana na ufadhili wa jumuiya ya Ulaya (EU) kwa kujenga vituo vya majaribio vya utafiti wa nishati ya jua na mawimbi ya bahari.

“Tunaendelea na kazi za utafiti wa nishati mbadala ambao utatuwezesha kuwa na vyanzo vyetu vya kuzalisha umeme kwa ajili ya maendeleo’alisema.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Ali Halik Mirza, alisema juhudi zinaendelea za kuhakikisha Zanzibar inapata nishati ya umeme mbadala itakayopunguza matumizi na kutegemea umeme kutoka Tanzania Bara kupitia Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).

“Kazi ya kutafuta nishati mbadala ya nguvu za umeme ni endelevu na muhimu kwa Zanzibar ili kuwa na umeme wake ambao unaweza kutumika wakati wa dharura,” alisema.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeanza kazi ya utafutaji nishati ya mafuta na gesi kufuatia Baraza la Wawakilishi kupitisha mswada wa mafuta na gesi na kutiwa saini na rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein.

Kampuni ya Bell Geospace kutoka Uingereza imepewa kazi ya kutafuta nishati ya mafuta na gesi kwa niaba ya kampuni ya Ras Gas kutka RasKhaimah.
chanzo:Habarileo.

Comments