Wananchi Kisiwani Pemba kupatiwa mifugo ili kujikimu kimaisha.

Image result for ng'ombe na mbuzi
Na Asha Salum.
SERIKALI  imedhamiria kuinua wananchi kiuchumi na kuondokana na utegemezi wa familia kwa kuwawezesha kuwapatia Ng’ombe wa maziwa wafugaji wadogo wadogo Kisiwani Pemba, jambo ambalo linawezekana iwapo wafugaji wenyewe watawatunza wanyama hao wakiwa na malengo yaliokudiwa.
Afisa Mkuu Idara ya maendeleo ya Mifugo Pemba, Asha Zahran Muhammed, ametoa maelezo hayo, wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, huko Ofisisni kwake, Mnazi Mmoja, Wilaya ya Wete, Mkoa wa Kaskazini .

Akieleza kuhusiana na dhana ya maendeleo ya mifugo, Asha Zahran amesema kuwa, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Idara husika imepanga kusimamia vyema ufugaji, kwa kuwapatia huduma stahiki wafugaji, ili waweze kuzalisha kwa wingi na kujiingizia kipato.
Hata hivyo, aliwataka wafugaji ambao wamebahatika kupata Ng’ombe hao kuwapa matunzo yanayostahiki kwa malengo yaliokusudiwa, ili na wengine waweze kusaidiwa kwa kuendeleza mradi uwe endelevu kwa faida ya wananchi wote na Taifa.
Akitoa shukurani kwa niba ya wafugaji wenzake katibu wa kikundi cha ufugaji wa Ng’ombe, Salim Sleiman Ali, kutoka kikundi cha Mkombozi, kilichopo Kisiwani kwa Bint Abeid, amesema kuwa, ni hatua kubwa iliofanywa na Serikali kuweza kuthamini hali za wananchi kwa kuwapatia mradi wa mifugo.
Salim amesema kuwa, dhamira ya Seriakali kwa Jamii ya wafugaji imeanza kupatikana kwani wameanza kuzalisha kwa kuuza bidhaa ya maziwa ambayo inawasaidia katika kuhudimia mifugo yao pamoja na baadhi ya huduma katika familia zao.
Akitaja matatizo yanayowakabili katika ufugaji amesema kuwa, ni pamoja na uhaba wa taaluma, bei kubwa ya vyakula vya mifugo, pamoja na uhaba wa madaktari unaopelekea kukosa huduma kwa wakati inapohitajika.
Aidha katibu huyo ameiomba Serikali kuzidi kuyaangalia kwa karibu matatizo yanayokwamisha juhudi zao na kuangali namna ya kuwasaidia kwa wakati muda unaporuhusu.
Takriban kipindi cha miaka mitatu iliopita 2014 hadi sasa, Serikali kupitia Mradi wa ASDP-L chini ya Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Kisiwani Pemba, Imeshatoa Ng’ombe wa Maziwa 180 wenye gharama ya Shilingi 36,000,000.
Vijiji vilivyopatiwa Ng’ombe hao ni Kangani, Mizingani, na Chokocho kwa Wilaya ya Mkoani, Vikunguni, Ole Jonwe kwa Wilaya ya Chake Chake, Kisiwani kwa Bint Abeid, na Piki kwa Wilaya ya Wete, Wingwi na Kinyasini kwa Wilaya ya Micheni ambapo kila kikundi kilipatiwa idadi ya Ng’ombne 20.

Comments